Arsenal, waliocheza ovyo FA wajiliwaza: ‘Hata kumbe tungepewa Man City nusu fainali’
WANAFAINALI wa Kombe la Shirikisho la Soka Uingereza (FA Cup) mwaka jana, Manchester City, watavaana na mabingwa wa mwaka 1976 Southampton katika nusu-fainali ya mwaka huu.
Nao mabingwa mara nane Chelsea watakabana koo na Leeds United katika nusu-fainali ya pili. Mechi hizo zote mbili zitasakatiwa uwanja wa Wembley wikendi ya Aprili 25-26.
Man City walinyorosha Liverpool 4-0 katika robo-fainali uwanjani Etihad mnamo Jumamosi kujizolea tikiti ya nusu-fainali, wakiweka rekodi ya kufuzu kwa awamu hiyo kwa msimu wa nane mfululizo.
Watakutana na Southampton kutoka daraja la pili Championship walioduwaza vinara wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Arsenal, kwa kuwalima 2-1 uwanjani St Mary’s mnamo Jumamosi usiku.
Southampton maarufu Saints walitwaa kombe hilo mwaka 1976 na watahitaji kutia bidii ya mchwa pamoja na kismati kudengua Man City ambao wanapania kufuzu kwa fainali ya nne mfululizo na kisha kuzoa kombe hilo kwa mara yao ya nane.
Jumapili, Leeds walijikatia tikiti ya kunogesha nusu-fainali ya FA kwa mara ya kwanza baada ya miaka 39 kufuatia ushindi wa 4-2 wa mikwaju ya penalti dhidi ya West Ham.
Penalti hizo zilihitajika kuamua mshindi baada ya mechi kutamatika sare ya 2-2 muda wa kawaida na wa ziada katika uwanja wa London Stadium.
Chelsea nao walinyeshea Port Vale kutoka daraja la tatu League One mvua ya mabao 7-0 katika robo fainali nyingine awali Jumamosi jioni.
Leeds walikuwa mbele 2-0 kupitia bao la Tanaka na penalti ya Dominic Calvert-Lewin dakika ya 26 na 75 mtawalia, lakini West Ham walirejea mchezoni dakika za majeruhi kupitia Mateus Fernandes (90+3) na Axel Disasi (90+6) na kuleta msisimko wa aina yake kwenye mchuano.
Kipa wa Leeds, Lucas Perri, ndiye aliibuka kuwa shujaa akiokoa penalti ya Jarrod Bowen na Pablo kupaisha waajiri wake hadi nusu-fainali, ambayo watanogesha kwa mara ya kwanza tangu 1987.
Aidha, wakishinda na kutua fainali watakuwa wakilenga kunyanyua kombe hilo kwa mara yao ya pili baada ya kuwa mabingwa 1972.
Mechi ya Leeds na mabingwa mara nane Chelsea itakuwa kumbukumbu ya fainali waliyosakata 1970 ambapo Chelsea waliibuka kidedea kutwaa kombe hilo.