Habari za Kaunti

Hofu Rais Ruto alitoa ahadi hewa kwa Wapwani kuhusu ardhi

Na WINNIE ATIENO April 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA mitatu baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2022, Rais William Ruto bado hajatatua mzozo wa muda mrefu wa ardhi katika eneo la Pwani licha ya kuahidi wakati wa kampeni akisaka kura za Wapwani.

Wakati wa kampeni, Rais aliahidi kushughulikia dhuluma za kihistoria za ardhi, ikiwemo kutenga fedha za kununua mashamba kutoka kwa wamiliki mabwanyenye ili kuzigawa kwa maskwota na kuwapa hatimiliki.

Rais aliteua viongozi wakuu wa Pwani akiwemo Spika wa Bunge la Seneti, Bw Amason Kingi, Waziri wa Madini, Bw Hassan Joho, na mwenzake wa Michezo na Vijana, Bw Salim Mvurya, ili kubaini na kujadiliana na wamiliki hao kuhusu mashamba hayo.

Hata hivyo, miaka mitatu baadaye, hatua chache zimepigwa huku maskwota wakiishi na wasiwasi wa kufurushwa kila uchao wakisubiri suluhisho kutoka kwa Rais.

Mawaziri Joho, Mvurya na Spika Kingi waliokabidhiwa jukumu la kubaini na kuchunguza wamiliki hao, wamekuwa wakizungumzia kuhusu jinsi Rais atakavyoshughulikia tatizo hilo la kihistoria, ikiwa imesalia miezi 16 kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Mwaka jana, wakati wa mazishi ya babake wa Spika Kingi, Mzee Kingi Mwaruwa Mkweha, huko Kamale, Magarini, Rais Ruto alisema serikali yake imepiga hatua katika kutatua changamoto za ardhi.

Serikali ilitenga Sh3.8 bilioni kwa ajili ya kununua ardhi kutoka kwa wamiliki mabwanyenye.

“Tumepiga hatua na sasa tuna fedha za kuwalipa wamiliki wasio wakazi,” alisema Rais, akieleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa kutatua matatizo ya ardhi yaliyodumu kwa karne nyingi na kuwaacha maelfu bila hati miliki.

“Haitakamilika kwa mwaka mmoja au miwili, lakini tutatekeleza ahadi yetu ya kutatua kwa kiasi kikubwa tatizo la maskwota Pwani,” alifafanua Rais Ruto.

Akizungumza na wakazi wa Ganze wiki iliyopita, Bw Kingi aliwataka wakazi wa Pwani kumrejesha Rais Ruto mamlakani kwenye uchaguzi mkuu wa 2027 ili kushughulikia changamoto za ardhi.

“Tumewaona marais wengi wakija Pwani wakituambia hadithi za ardhi zetu, hadithi zisizo na kichwa wala miguu, wakitudanganya. Lakini Rais Ruto, ambaye hata alikuja kutangaza mipango yake, alisema ataanza mpango maalum kushughulikia tatizo sugu la ardhi,” alisema Bw Kingi.

Spika huyo alisema alipokuwa gavana wa Kilifi kwa miaka 10, mara kwa mara alikuwa akipokea taarifa za kufurushwa kwa wananchi na kubomolewa nyumba zilizojengwa kwenye mashamba yaliyokuwa na mizozo.

Alisema kabla hajashirikiana na chama tawala cha UDA, Rais alimhakikishia kuwa swala la ardhi litashughulikiwa kikamilifu.

“Ninataka kutangaza hapa Ganze kwamba Rais tayari amefanya mazungumzo na matajiri wa ardhi wanaomiliki mashamba makubwa Pwani. Wamekubaliana kuhusu bei. Serikali itanunua mashamba hayo na kugawa kwa maskwota. Rais ameahidi kurejesha heshima yetu ili tusibaki bila makazi. Hii ni hatua kubwa ambayo haijawahi kutokea,” alisema Bw Kingi.

Alisisitiza kuwa kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto kutahakikisha wakazi wa Pwani wanapata ardhi yao.

Hata hivyo, mashirika ya kiraia yamebaki na mashaka. Afisa wa Kenya Land Alliance, Bw Nagib Shamsan, alisema bado wanasubiri ahadi ya Rais itekelezwe kabla ya uchaguzi mkuu.

“Tuna hofu kama wenyeji kwamba tangu ahadi hiyo, hakuna kilichotekelezwa. Tunapoelekea uchaguzi mkuu, je, wagombea urais watatumia tena suala la ardhi kama chambo cha kuwashawishi wananchi?” aliuliza Bw Shamsan.

Changamoto za kihistoria za ardhi, kufurushwa kwa wananchi na tatizo la maskwota zimekuwa donda sugu pwani kwa miongo mingi, huku wanasiasa wakilitumia kufanyia kampeni.

Ingawa viongozi wa Pwani wamelipongeza jambo hilo wakisema Rais atatatua changamoto hizo, wakazi wengi bado wana tahadhari.