Lugha, Fasihi na Elimu

Ili kukuza Kiswahili kwa kasi zaidi, ushindani kati ya Kenya na Tanzania ukumbatiwe

Na PROF IRIBE MWANGI April 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MNAMO Aprili 1, shirika la NASA lilituma chombo angani kuelekea mwezini.

Kwa muda wa siku kumi, chombo hicho kilichopewa jina Orion kimekuwa na jukumu la kukusanya habari kuhusu mwezi na anga.

Wanaanga wenye jukumu hilo katika mradi huo uitwao Artemis II ni Reid Wiseman, Victor Glover, Christina Koch na Jeremy Hansen.

Safari hii inafikia umbali ambao haujawahi kufikiwa na binadamu.

Pili, wanaanga hawa wameweza kuona upande wa mwezi ambao haujawahi kuonekana tena na binadamu. Upande huo una milima ya miamba na mabonde makubwa.

Inakisiwa kwamba mradi huu utasaidia katika kumwezesha binadamu kufikia sayari ya Mirihi (Mars) inayodhaniwa kuwa na madini mengi.

Hatua hizi muhimu katika ugunduzi zimefikiwa kutokana na mashindano baina ya mataifa mbalimbali.

Mnamo 1959 katika mradi ulioitwa Luna 2, Muungano wa Sovieti ulituma chombo mwezini.

Mnamo 1966, chombo kilichoitwa Luna 9 kilitua mwezini. Hali hii iliwapa washindani wa Sovieti, yaani Marekani, kiwewe.

Kufikia mwisho wa muongo wa 60, mnamo 1969 katika mradi ulioitwa Apollo 11, Marekani ilifaulu kuwatuma wanaanga watatu mwezini ambapo Neil Armstrong na Buzz Aldrin waliandika historia kama binadamu wa kwanza kukanyaga na kutembea mwezini.

Mwenzao Michael Collins alisalia chomboni kwa kuwa ndiye aliyekuwa rubani.

Wanaanga wa Apollo 17 ya Marekani walitua mwezini mnamo 1972 na Wasovieti katika Luna 24 wakawa wa mwisho kufika mwezini katika milinia hiyo mnamo 1976.

Muungano wa Sovieti ulisambaratika mnamo 1991. Hali yake ya udhaifu ilikuwa imeanza katika miaka ya 80.

Kwa kukosa ushindani, safari za kuenda mwezini zilikoma. Ndio sababu imekuwa miaka 54 tangu Wamerekani walipofika mwezini mara ya mwisho.

Lakini sasa mambo yamebadilika. Kuna ushindani mpya. Nchi ya Uchina ina mradi unaoitwa Chang’e na ina lengo la kupeleka wanaanga mwezini kufikia 2030.

Mnamo 2019, kwa kutumia roboti kwenye Chang’e 4, Uchina lilikuwa taifa la kwanza kufika eneo la mbali kabisa la mwezi. Baada ya hapo, roboti za Wachina zilifanya ziara mnamo 2020 na 2024.

Ni maoni yangu kwamba ziara hizi za Wachina ndizo zilizogutua Marekani na kwa sasa ni wazi kwamba ushindani umeanza rasmi!

Ushindani

Nimeandika haya kudhihirisha kwamba ushindani baina ya mataifa aghalabu huzaa matunda mema.

Ni kwa mintarafu hii ndipo ninapendekeza kwamba kuwe na ushindani wa kina baina ya Kenya na Tanzania katika kukuza na kusambaza Kiswahili.

Ushindani huu utakuwa baraka kuu kwa lugha yenyewe.

Nchi ya Tanzania imefanya mengi katika kukuza Kiswahili nyumbani na kimataifa. Ni maoni yangu kwamba iwapo kungekuwa na ushindani katika hili, basi kazi ya kukikuza na kukisambaza ingeongezeka.

Kuhusu Kiswahili, mshindani wa pekee wa Tanzania ninayemwona ni Kenya.

Kenya inafaa itie nia na ionyeshe ari kushindana na Tanzania katika kuasisi vituo vya kufunza Kiswahili katika mabalozi yake.

Vilevile, Kenya inafaa kushindana na Tanzania katika shughuli za kibalozi za utambuzi wa Kiswahili.

Iwapo Tanzania ilishirikiana na UNESCO ili kuamuliwa kuwe na Siku ya Kiswahili Duniani, Kenya inaweza kufanya nini?

Vilevile, Kenya inafaa kushindana na Tanzania katika kutuma walimu wa Kiswahili katika mataifa mbalimbali ya Afrika na nje ya bara hili.

Zaidi ya yote, Kenya inafaa kushindana na Tanzania katika kuzindua taasisi na asasi tofauti tofauti zitakazokuza Kiswahili.

Nchini Tanzania kuna mabaraza mawili ya Kiswahili (BAKITA na BAKIZA) ilhali Kenya hakuna hata moja.

Tanzania kuna taasisi ya masomo ya Kiswahili (TATAKI) ilhali Kenya hatuna taasisi kama hiyo.

Kwa hakika, nimeelezwa kwamba serikali ya Tanzania imetoa ardhi ya kujenga chuo kikuu kitakachotambulika na kuimarika katika ufunzaji wa Kiswahili, Kenya je?

Naomba nchi yetu ishindane na jirani wetu kwa hili. Huu utakuwa ushindani chanya.