Habari za Kitaifa

Uhaba wa mafuta waanza kuripotiwa maeneo mbalimbali nchini

Na WAANDISHI WETU April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAENEO kadhaa nchini yanakabiliwa na uhaba wa mafuta huku ikihofiwa kwamba wafanyabiashara wanahodhi bidhaa hiyo.

Kero hiyo inayohusishwa na utatizwaji wa soko la dunia huku taharuki ikizidi kutanda Mashariki ya Kati kutokana na vita vya Amerika na Israeli dhidi ya Iran, imeathiri zaidi kampuni huru za mafuta, huku vituo vingi vya mafuta, hasa maeneo ya mashinani yakiripoti uhaba wa bidhaa.

Haya yanajiri hata baada ya taasisi za kiserikali na wadhibiti kuhakikishia umma mara kadhaa kwamba nchi ina hifadhi ya kutosha ya mafuta na hakuna upungufu.

Katika eneo la Mlima Kenya, upungufu umeripotiwa katika kaunti za Muranga, Meru, Nyeri, Kirinyaga na Embu.

Bidhaa za dizeli na petrol ziliadimika Murang’a ambapo ni vituo vya Rubis na Shell pekee vilikuwa na bidhaa chache.

Jana na Jumanne, foleni ndefu zilishuhudiwa katika vituo vya mafuta mijini Chuka, Embu, Meru, Nanyuki na Isiolo huku waendeshaji magari waking’ang’ania tone la mwisho la mafuta.

Katika kaunti za Kirinyaga na Embu, uhaba huo ulizua taharuki ya ununuzi ambapo waendeshaji magari na bodaboda walipanga foleni ndefu katika vituo vya petrol.

Uhaba wa mafuta umelemaza magari ya umma na ya kibinafsi huku mengi yakionekana kukaa bure maegeshoni au kuachwa katika vituo vya petroli katika kaunti za Nyandarua na Laikipia.

Uchunguzi uliofanywa maeneo ya Kitale, Kiminini, Kachibora na Endebess, Kaunti ya Trans Nzoia ulifichua uhaba huku baadhi ya vituo vikifungwa na vingine kuzidiwa na wateja.

Jijini Kisumu, waendeshaji magari wanakabiliwa na uhaba wa bidhaa za mafuta zinazodidimia huku wakionya kuwa bidhaa zilizosalia hazitadumu zaidi ya wiki moja.

Mjini Nyamira, Joshua Omasire alisimulia masaibu yake baada ya kusaka mafuta kwa siku mbili bila mafanikio.

Eldoret, Uasin Gishu na viungani mwake kuna uhaba wa mafuta ambapo baadhi ya vituo havina petroli au dizeli.

Pwani, madereva wa masafa marefu walielezea wasiwasi kuhusu uhaba wa mafuta wanaosema unatishia usafirishaji wa mizigo nchini na Afrika Mashariki.

Hata hivyo, bidhaa za mafuta zimerejea kaunti za Bomet, Kericho, na Narok siku moja tu baada ya uhaba kuripotiwa katika vituo vingi.

Mwenyekiti wa Muungano wa Wasafirishaji Newton Wang’oo amesema katika siku chache zilizopita, wasafirishaji kote nchini, hasa kwenye mikondo muhimu ya usafiri, wameshuhudia uhaba wa mafuta kutokana na wauzaji kukataa kuwasilisha shehena na kampuni za mafuta kuondoa mikopo.

“Sekta ya usafiri wa barabara ni uti wa mgongo wa uchumi wa Kenya na biashara katika jumuiya ya Afrika Mashariki. Hali ya sasa inatishia usafirishaji wa bidhaa muhimu, ustawi wa michakato ya usambazaji bidhaa na nafasi ya Kenya kama kituo kikuu cha usafirishaji,” alisema Bw Wang’oo.

Kwingineko, bidhaa za mafuta zilijazwa upya katika miji ya Narok na Kericho ikiwemo vituo vya kibiashara vya Litein, Kapsoit, Kapkatet, Sotik, Mulot, Ololulunga, na Sogoo.

Jijini Nairobi, vituo vingi vilikuwa na mafuta.

Baadhi ya vituo Westlands, Lang’ata, Mombasa Road, Nairobi ya kati viliendelea kuuza mafuta vikiwa na foleni fupi.

Martin Chomba wa Muungano wa Vituo vya Petroli alieleza Taia Leo kwamba vituo vya petrol visivyo na bidhaa za kutosha vitalazimika kustahimili hali.

Ikiwa vituo vidogo vya petrol viungani mwa Kenya vinalalamikia upungufu wa mafuta,” alisema Chomba “vituo vya petrol visivyo na uhaba wa mafuta vitahitajika kustahimili hali huku wateja zaidi kutoka mashinani wakipanga foleni kununua mafuta.”