Ruto: Nitawanyamanzisha wakosoaji wangu
RAIS William Ruto amesema serikali yake itatekeleza miradi ya maendeleo ili kujibu wakosoaji wanaomshutumu kwa kutoa ahadi zisizotekelezeka.
Akizungumza Taita Taveta, Rais alisema serikali imetenga fedha za kujenga barabara ya Mtomwagodi–Msau–Dawida–Mbale–Wundanyi hadi Bura, ambayo imekuwa ikisubiriwa kwa miongo kadhaa.
“Nitawajibu wakosoaji kwa vitendo, si maneno,” alisema.
Aliongeza kuwa kilomita 20 za barabara ya kuunganisha Taita Taveta na Kajiado zimekamilika, huku zilizobaki zikitarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka.
Miradi hiyo, alisema, itaimarisha biashara, usafiri na kilimo.
Rais pia alitangaza mpango wa kufufua reli ya zamani kutoka Voi hadi Holili kwa gharama ya Sh5 bilioni ili kuimarisha biashara kati ya Kenya na Tanzania. Reli hiyo itapanuliwa hadi Taveta na baadaye kuunganisha ukanda wa Afrika Mashariki.
Aliwataka wanasiasa kuacha siasa za mgawanyiko, akisisitiza umuhimu wa umoja wa kitaifa kupitia serikali ya “broad-based”.
Gavana Andrew Mwadime alimpongeza Rais, akisema miradi hiyo itachochea maendeleo ya uchumi wa kaunti.