Dondoo

Waumini wazuia polo kutoa dozi ya mnazi kama fungu la kumi kwenye madhabahu

Na KALUME KAZUNGU April 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MATSANGONI, Kilifi:

IBADA katika kanisa moja kijijini hapa, ilisitishwa kwa muda waumini walipomzuilia polo kukaribia madhabahu akiwa amebeba jerikeni lililojaa pombe ya mnazi kuitoa fungu la kumi.

Polo huyo aliingia ghafla kanisani wakati ibada ikiendelea huku akiwa amejitwika kichwani jerikeni iliyojaa mnazi uliosababisha harufu kutapakaa kila mahali ndani ya kanisa hilo.

Bila kupoteza muda, jamaa alifululiza moja kwa moja kuelekea madhabahuni ambako pasta alikuwa akiendeleza mahubiri.

Hali hiyo iliwafanya baadhi ya waumini kumkimbilia buda huyo, kumshika mkono na kumrai waandamane nje.

Jamaa alidinda na kuwaambia waliomshika wamwache angalau afike mbele ya madhabahu ambako pasta alikuwa.

Aliwaeleza kuwa azma yake ya kuingia kanisani ilikuwa ni kutoa fungu la kumi.

“Mniache nipeleke hili fungu langu la kumi. Msinizuie,” akafoka.

Ni hali iliyowaacha waumini wengi wakishangaa huku pasta akiagiza waliojaribu kumzuia wamwache akaribie alipokuwa amesimama.