Habari za Kitaifa

Watu wangu msilipize kisasi, Kalonzo arai wakazi kuhusu mauaji

Na PIUS MAUNDU May 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Kiongozi wa chama cha Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka, amewataka wakazi wa Kaunti ya Kitui kujizuia kulipiza kisasi kufuatia mashambulizi yanayodaiwa kufanywa na wafugaji wa ngamia kutoka kaunti ya Tana River.

Akizungumza wakati wa mazishi ya pamoja ya wakazi saba waliouawa kwa kupigwa risasi katika eneo la Kwa Kamari, Kaunti ndogo ya Tseikuru, Bw Musyoka alisema kulipiza kisasi kunaweza kuleta madhara zaidi kwa jamii ya Wakamba wanaoishi maeneo mengine ya nchi na pia kuathiri malengo yake ya kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027.

Waliouawa ni Kilonzo Kauni, Mulandi Kauni, Mutua Kituo, Syengo Mwangangi, Damaris Matei, Nicholas Muthi Syengo na Tito Munywoki Muthi. Mauaji hayo yalitokea siku mbili tu kabla ya mvulana wa miaka 14, Joseph Mutemi, kuuawa kwa kukatwakatwa katika eneo la Ukasi.

Naibu Kamishna wa Kaunti ndogo ya Tseikuru, Anita Mwangi, alisema mashambulizi hayo yamezidisha hofu na taharuki katika eneo la mpakani kati ya Kitui na Tana River.

Bw Musyoka alitumia hafla hiyo kukosoa serikali ya Rais William Ruto akisema hali ya usalama eneo hilo inaonyesha udhaifu wa uongozi wa sasa.

“Msikate tamaa. Ndani ya chini ya mwaka mmoja na nusu, kwa mapenzi ya Mungu, upepo wa kisiasa utabadilika na matatizo haya yatakuwa historia,” alisema.

Aliwasihi wakazi kutojihusisha na mashambulizi ya kulipiza kisasi akisisitiza kuwa hatua hiyo inaweza kuzua madhara makubwa zaidi.

“Najua ni rahisi kupanga kulipiza kisasi, lakini nawasihi msifanye hivyo. Mungu atatulipizia,” aliongeza.

Kiongozi huyo pia alitoa wito wa mazungumzo kati ya jamii zilizoathirika na wanaodaiwa kutekeleza mashambulizi hayo. Alimpongeza Gavana wa Kitui, Julius Malombe, kwa kuanzisha juhudi za mazungumzo na mwenzake wa Garissa, Nathif Jama, ili kumaliza migogoro kati ya wakulima na wafugaji wa ngamia.

Wakati huo huo, Bw Musyoka aliwataka wakazi wa Ukambani kujitokeza kuendelea kujisajili kama wapigakura ili kupiga jeki azima yake ya kisiasa katika uchaguzi wa 2027 iwapo atakuwa mgombea wa urais wa upinzani.