Teknolojia mpya ya “genome editing” yazidi kushika kasi, mjadala wa GMO ukiendelea
MJADALA kuhusu mazao yaliyoboreshwa vinasaba (GMO) ukiendelea nchini, teknolojia mpya ya kuhariri vinasaba—genome editing, inaanza kujitokeza kama suluhu mbadala inayoweza kubadilisha mustakabali wa kilimo Kenya.
Kenya, kama mataifa mengine ya Ukanda wa Pembe ya Afrika, imeathirika pakubwa na mabadiliko ya tabianchi, hali inayolazimu mageuzi ya haraka katika mifumo ya uzalishaji chakula.
Ili kukabiliana na hali hiyo, sekta ya kilimo imeanza kuangazia mbinu bunifu zinazoongeza uzalishaji na kustahimili misukosuko ya hali ya hewa.
Kwa muda, teknolojia ya GMO imekuwa kitovu cha mjadala. Licha ya changamoto za kisheria, Kenya tayari iliidhinisha kilimo cha pamba iliyoboreshwa kisayansi—Bt cotton, mwaka 2019, aina inayostahimili wadudu waharibifu na kuongeza mavuno.
Hata hivyo, hatua ya kuondoa marufuku ya GMO iliyotangazwa mwaka 2022 ilisimamishwa na mahakama kufuatia kesi zilizowasilishwa na wapinzani wa teknolojia hiyo.
Mahindi ya GMO, hususan Bt maize, pia yako katika hatua za mwisho za majaribio ya kitaifa, yakilenga kukabiliana na wadudu waharibifu na magonjwa hatari. Lakini mvutano wa kisheria umeendelea kuchelewesha utekelezaji wake.
Ni katika muktadha huu ndipo genome editing inaibuka. Tofauti na GMO, teknolojia hii haileti jeni (genes) kutoka kwa kiumbe kingine. Badala yake, hubadilisha au kupanga upya vinasaba vya mmea wenyewe ili kuboresha sifa muhimu kama uzalishaji, kinga dhidi ya magonjwa na uwezo wa kustahimili ukame.

Anne Muia, mwanasayansi kutoka Mamlaka ya Kitaifa ya Usalama wa Kibayolojia (NBA), anasema mabadiliko ya vinasaba hutokea kiasili, lakini teknolojia mpya kama CRISPR-Cas9 imewezesha kuyafanya kwa haraka na kwa usahihi mkubwa.
“Badala ya kusubiri mabadiliko ya kiasili kwa miaka mingi, sasa tunaweza kurekebisha vinasaba kwa njia inayolenga matokeo mahususi,” anasema. Kenya imekuwa ikiwekeza katika utafiti wa genome editing kwa takriban miaka mitano sasa. Katika Chuo Kikuu cha Kenyatta, watafiti wanaendeleza tafiti kuhusu mboleahai na uboreshaji wa mazao kwa kutumia teknolojia hii.
Profesa Richard Oduor, mtaalamu wa Bayolojia ya Molekuli na Seli, anasema tofauti kuu kati ya GMO na genome editing ni chanzo cha vinasaba vinavyotumika. “Katika GMO, jeni kutoka spishi nyingine huingizwa kwenye mmea. Hii ilizua hofu miongoni mwa umma kuhusu vinasaba vya kigeni. Lakini katika genome editing, mmea huboreshwa kwa kutumia vinasaba vyake wenyewe,” anafafanua.
Anaongeza kuwa teknolojia hiyo inafanya kazi kama “makasi ya molekuli”, ambapo sehemu maalum ya DNA hukatwa na kurekebishwa ili kutoa sifa bora zaidi.
Tayari, mazao yaliyohaririwa vinasaba kupitia genome editing yanapatikana sokoni katika baadhi ya mataifa, huku Amerika na China zikiongoza katika matumizi ya teknolojia hiyo.
Barani Afrika, nchi kama Afrika Kusini, Nigeria na Ghana zimeanza kuikumbatia, zikichochewa na uzoefu wao wa awali na GMO.

Nchini Kenya, tafiti zinaendelea kwa mazao mbalimbali. Kulingana na Anne Muia, kuna majaribio ya mtama unaostahimili magonjwa hatari kama striga, mpunga unaojikinga dhidi ya magonjwa ya fangasi, na mahindi yanayostahimili ugonjwa wa maize lethal necrosis.
“Striga, maarufu kama witch weed, ni tishio kubwa kwa mazao ya nafaka kama mahindi, mtama na mpunga, na husababisha hasara ya mabilioni ya fedha kila mwaka Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara,” Anne anaonya.
Kulingana na Prof Oduor, genome editing ina uwezo mkubwa kuimarisha usalama wa chakula na kuchochea ukuaji wa uchumi. Hata hivyo, anasisitiza umuhimu wa uelewa wa umma na mifumo madhubuti ya usimamizi ili kuhakikisha teknolojia hiyo inakubalika na kutumika ipasavyo.
Kadri changamoto za tabianchi zinavyozidi kuongezeka, teknolojia kama hizi zinaweza kuwa nguzo muhimu katika kulinda uzalishaji wa chakula nchini—zikitoa matumaini mapya kwa wakulima na mustakabali wa kilimo Kenya.