Habari

Polisi wachunguza madai shirika linahusika na ulanguzi, unyanyasaji wa watoto Mombasa

Na BRIAN OCHARO May 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAAFISA wa Kitengo cha Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu na Kulinda Watoto wanachunguza mtindo unaodaiwa kuwashawishi na kuwasafirisha watoto kushirikishwa katika unyanyasaji wa kingono kwa kisingizio cha kuwapa ufadhili na kukuza vipaji vyao katika kaunti ya Mombasa na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa stakabadhi zilizowasilishwa mahakamani, genge hilo linafanya shughuli zake kupitia shirika lililojulikana kama “Talanta ni Kazi”, maarufu pia kama “Talent ni Kazi” na “Ribe Rescue Youth”, ambalo linadaiwa kuanzishwa na kuendeshwa na Almasi Rama Amos anayefahamika pia kwa jina la Mjanja Almasi.

Wachunguzi wanasema wasichana wadogo kutoka familia maskini na mazingira duni walivutwa kwa ahadi za masomo, kukuzwa vipaji na kusaidiwa kimaisha, lakini baadaye wakageuzwa waathiriwa wa usafirishaji haramu na dhuluma za kingono.

“Uchunguzi wa awali umebaini kuwa mshukiwa pamoja na washirika wake waliwatafuta, waliwahifadhi, waliwasafirisha na kuwaficha watoto hao kabla ya kuwafanyia vitendo vya unyanyasaji ,” alisema afisa mpelelezi Hillary Serem .

Hati za mahakama zinaeleza kuwa mshukiwa aliwavutia wazazi na walezi kwa kujitambulisha kama mfadhili na mlezi wa vijana kupitia mipango ya vipaji na uwezeshaji wa watoto wenye changamoto za maisha.

Polisi walieleza kuwa watoto 19 waliokolewa Mei 7 katika operesheni zilizofanywa Bamburi na Kambe-Ribe. Watoto watatu walipatikana katika eneo la Ngu Tatu, Bamburi-Ugatuzi huku wengine 16 wakiokolewa Kambe-Ribe.

Maafisa hao pia walinasa simu za mkononi, kadi za simu , kompyuta na vifaa vingine vya kielektroniki vinavyoaminika kuwa na ushahidi muhimu kuhusu mtandao huo.

“Baadhi ya waathiriwa walikatiza masomo yao walipokuwa chini ya usimamizi wa mshukiwa,”afisa huyo alisema.

Wachunguzi pia wanadai baadhi ya watoto hao walipata ujauzito baada ya kudhulumiwa kingono mara kwa mara.

Polisi sasa wanaomba mahakama iwape muda zaidi wa kumzuilia mshukiwa ili kukamilisha uchunguzi, uchambuzi wa kisayansi na kuwatafuta washukiwa wengine pamoja na waathiriwa ambao bado hawajapatikana.