Wito serikali ihakikishe watoto wote wanapata elimu bila ubaguzi
KINARA wa chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka, ameihimiza serikali kuhakikisha kila mtoto nchini anapata elimu bila vikwazo, akisema wanafunzi wengi kutoka familia maskini wanatatizika kuendelea na masomo kutokana na ukosefu wa karo na ufadhili wa kutosha.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Lizah Foundation International jijini Nairobi, Kalonzo alisema elimu ni haki ya msingi ambayo serikali inafaa kuipa kipaumbele ili kusaidia watoto kufikia ndoto zao.
“Ni jambo la kuhuzunisha kuona wanafunzi wengi wakikosa kuendelea na masomo kwa sababu ya changamoto za kifedha. Serikali inapaswa kutenga rasilimali za kutosha katika elimu. Ninaona roho ya Wangari Maathai ndani ya Lizah, na naamini taasisi hii itafika mbali katika kusaidia wasiojiweza,” alisema Kalonzo.
Waziri wa Kawi, Opiyo Wandayi, alisema serikali ya Kenya Kwanza itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo kwa usawa kote nchini bila ubaguzi wa kikabila au kisiasa.
“Nchi hii ni ya Wakenya wote, na maendeleo yatagawanywa kwa usawa katika maeneo yote,” alisema Wandayi.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Ouma Oluga, alisema wizara hiyo itashirikiana na taasisi hiyo kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya afya na ustawi.
Lizah Foundation International, inayoongozwa na aliyekuwa mwanahabari Lizah Mutuku, imekuwa mstari wa mbele kusaidia miradi ya mazingira, elimu kwa watoto wanaotoka katika familia maskini na kuwawezesha wasichana kufanya maamuzi bora maishani.
Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni pamoja na Ezekiel Mutua, wabunge, wanahabari na viongozi mbalimbali wa kijamii.