Habari

Arati, Bosire wachanganyikiwa, hawajui wamuunge Ruto au Matiang’i

Na RUTH MBULA May 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha ODM kinaonekana kuwa na kibarua kudumisha umaarufu wake eneo la Gusii kutokana na nia ya Dkt Fred Matiangí ya kutaka kuwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Gavana wa Kisii, Simba Arati na aliyekuwa Mbunge wa Kitutu, Masaba Timothy Bosire ndio nyapara wa ODM eneo la Gusii.
Bw Bosire pia ni mwekahazina wa ODM.

Kutokana na umaarufu wa Dkt Matiangí eneo la Gusii, viongozi wa ODM wapo njia panda iwapo wataendelea kuunga azma ya Rais Ruto na kuhatarisha viti vyao au wajiunge na mrengo wa upinzani.

Bw Arati na Bw Bosire wameonekana kuwa vuguvugu na kutatizika kuchukua msimamo kuhusu iwapo watamuunga Dkt Matiangí au wataendelea kurindima ngoma ya ‘Tu Tam’.

Wabunge wengi wa ODM kutoka kaunti za Kisii na Nyamira washahamia kambi ya Dkt Matiangí.

Wao ni Seneta wa Nyamira Okongó Omogeni, mwenzake wa Kisii Richard Onyonka na wabunge Anthony Kibagendi (Kitutu Chache Kusini), Obadiah Barongo (Bomachoge Borabu), Clive Gisairo (Kitutu Masaba) na Patrick Osero (Borabu.

Wikendi iliyopita Mabw Arati na Bosire waliyatoa matamshi ambayo yanaweza kufasiriwa kuwa wanachangamkia mrengo wa Dkt Matiangí.

Walikuwa wamemtembelea Bw Onyonka ambaye anaendelea kuomboleza kifo cha mamake.

Bw Arati alidai kuwa ni ‘mwendawazimu’tu atakosa kuunga azma ya urais ya Dkt Matiangí.

“Huu mradi wa Matiangí ni wangu. Muulize, kisha uwaulize Mzee Profesa Sam Ongeri, Mzee John Simba na Mzee Omenge. Mara ya kwanza aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alianza kuanza kumhangaisha Matiangí, mimi ndiye aliniambia niingie kati na nimtetee kwa Rais Ruto,” akasema Bw Arati.

“Tulipofika katika afisi ya rais, ni mimi nilimwaambia rais aliyekuwa na hasira akomeshe kuhangaishwa kwa Matiangí,” akaongeza.

Bw Arati amekuwa akiegemea kwenye mrengo wa Rais Ruto na alisema kuwa eneo la Gusii litakuwa nyuma ya Dkt Matiangí iwapo atakuwa debeni hadi mwisho.

Mwanzoni Bw Arati alichangamkia Dkt Matiangí lakini baadaye akalegea na kuendelea na siasa za kuunga azma ya Rais Ruto.

“Kinyume na vyeo vingine, nafasi ya ugavana lazima uwe makini jinsi ambavyo utacheza siasa zako. Hata miradi ambayo inastahili kutekelezwa inaweza kusitishwa,”akasema

Gavana huyo aliitaka jamii ya Gusii isalie kama imeungana akisema kuwa hata katika uchaguzi mkuu wa 2022 hakuna aliyetarajia kuwa Rais Ruto angeingia afisini.

“Najua Onyonka anataka kuwania ugavana na namkaribisha kwa sababu kila mtu ana ndoto zake. Pia nimewaona wanawake wengi wanataka wadhifa huu, sote tunalenga uongozi bora,” akasema.

Bw Bosire naye aliwataka viongozi kutoka eneo la Gusii wakome kumvamia Dkt Matiangí.

Alisema waziri huyo wa zamani anahitaji kulindwa kwa sababu anatoka eneo la Gusii huku akimpa Dkt Matiangí moyo aendelee kupambana.

“Sote tunatoka jamii ya Fred Matiangí, tusiwe wa kwanza kumvamia. Wengine waongee lakini sisi tumlinde,” akasema Bw Bosire.