Hofu mgawanyiko wa upinzani utapatia UDA ushindi Ol Kalou
HATUA ya chama cha Jubilee kusimamisha mgombea wake katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou unaotarajiwa Julai imeonekana kutikisa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), kinachoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Muungano huo wa upinzani,unahofia kuwa vyama hivyo, vinaweza kugawanya kura na kupatia chama cha United Democratic Alliance (UDA) ushindi kirahisi.
Chama cha People’s Liberation Party kinachoongozwa na Martha Karua, ambacho pia ni sehemu ya muungano huo, kimemteua Martin Wambugu kuwania kiti hicho.
Hali imekuwa ngumu zaidi baada ya wagombeaji wote wa Jubilee na UDA walioshindwa kwenye kura za mchujo kutangaza kumuunga mkono mgombea wa chama chao, huku wagombeaji watatu pekee kati ya wanane wa DCP wakikubali kumuunga mkono mshindi Kamau Ngotho.
Bi Beatrice Kamau na Bw Isaac Wanjiru waliokuwa wamejitosa kwenye kura za mchujo za Jubilee, walisema wanaunga mkono uamuzi wa chama hicho kumpa tiketi Mhandisi Wilson Kigwa.
Bi Kamau alisema tayari amekubaliana na Bw Kigwa kwamba angempa nafasi wakati huu kwa kuwa alikuwa amejiandaa zaidi kisiasa.
“Nilihisi sikuwa tayari kikamilifu kwa uchaguzi huu mdogo ambao ulitangazwa ghafla baada ya kifo cha marehemu David Kiaraho. Nitamuunga mkono mgombea wa Jubilee kwa sababu nina imani na chama hicho,” alisema.
Bw Wanjiru naye alisema atamuunga mkono Bw Kigwa huku akijiandaa kwa uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.
Wachambuzi wa siasa wanasema idadi ya wapiga kura waliojitokeza katika kura za mchujo haiwezi kutumika kutabiri matokeo ya uchaguzi mdogo wa Julai 16.
Wanasema kuna uwezekano hata mgombea huru au wa chama kidogo kushinda kutokana na mgawanyiko uliopo.
Sababu nyingine inayotajwa ni siasa za ndani za eneo hilo ambazo zinaweza kuathiri uchaguzi huo licha ya umaarufu ambao DCP inadaiwa kuwa nao.
Aliyekuwa waziri Maina Kamanda, alisema DCP inataka kuepuka migogoro ya ndani iliyogharimu Jubilee katika uchaguzi mdogo wa Rurii mwaka 2021 na uchaguzi mkuu wa 2022.
Katika uchaguzi mdogo wa Rurii, makundi mawili yaliyokuwa yakimuunga mkono mgombea wa Jubilee yalijitokeza, moja likiongozwa na aliyekuwa gavana Francis Kimemia na jingine na aliyekuwa Waziri Sicily Kariuki.
Migogoro hiyo ilipelekea mgombea wa UDA Francis Muraya Githaiga kushinda na kuwa kiongozi wa kwanza wa UDA kuchaguliwa Nyandarua.
Mvutano huo uliendelea hadi uchaguzi mkuu wa 2022 wakati Bi Kariuki alikataa kufanya kampeni za pamoja na Bw Kimemia.
Sasa siasa hizo zimeibuka tena katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.
Bw Kimemia anamuunga mkono mgombea wa Jubilee Wilson Kigwa, huku Bi Kariuki akimuunga mkono mgombea wa DCP Kamau Ngotho.
Mwakilishi wa wanawake Faith Gitau, ambaye pia anawania ugavana wa Nyandarua mwaka 2027, anamuunga mkono mgombea wa UDA Muchina Nyaga.
Bi Gitau alisema UDA haitakumbwa na migogoro ya ndani kwa sababu yeye ndiye mgombea pekee wa ugavana ndani ya chama hicho.
Alisema UDA itashinda uchaguzi huo kwa kishindo licha ya DCP kudai kupata idadi kubwa ya wapiga kura katika kura za mchujo.
Naibu kiongozi wa Jubilee Jeremiah Kioni alitilia shaka uhalali wa kura za mchujo za DCP akisema kila mtu aliruhusiwa kupiga kura bila kuwa mwanachama rasmi wa chama hicho.
Kwa upande mwingine, DCP ina wagombeaji watatu wa ugavana wanaotumia uchaguzi huo kujitangaza kisiasa.
Bw Kamanda alisema viongozi hao wanapaswa kufanya kazi pamoja ili kuepuka migawanyiko iliyowahi kuangusha Jubilee.
Bw Kimemia alikiri kuwa migogoro ya ndani iligharimu Jubilee katika chaguzi zilizopita lakini akasema kwa sasa anajikita katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.