Habari za Kitaifa

Gachagua: Msitutishe eti mtaiba kura mkishindwa 2027, mtaiba tukiwa wapi?

Na ERIC MATARA, MERCY KOSKEI May 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KINARA wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua amepuuzilia mbali hofu kuhusu wizi wa kura kabla ya Uchaguzi Mkuu 2027 akisema ni jambo lisilowezekana.

Bw Gachagua, aliyezungumza Nakuru wakati wa ibada ya mazishi ya mchungaji Catherine Macharia, mkewe askofu wa kanisa la Full Gospel Churches of Kenya, David Macharia, alitaja vitisho vilivyotolewa majuzi na wandani wa Rais William Ruto kuwa hewa.

Naibu Rais huyo wa zamani alisema marekebisho ya sheria kuhusu kuhesabu kura kutoka vituo vikuu hadi vituo vya kupigia kura yaliziba nyufa za udanganyifu.

“Serikali ya Rais Ruto na wandani wake hawawezi kuiba uchaguzi. Haiwezekani,” alisema Bw Gachagua.

“Nimesikia wandani wa Rais Ruto wakifananisha Kenya na nchi nyinginezo za Afrika Mashariki kama vile Tanzania, lakini nataka kuwahimiza Wakenya wasiwe na hofu kuhusu hilo. Hakuna yeyote atakayeiba kura. Wanawezaje kuiba kura? Tutalinda kura zetu. Haiwezekani; hivyo ni vitisho hewa.”

Bw Gachagua vilevile alisema Rais Ruto atashindwa kwa kura chungunzima na kwa kiwango hicho, udanganyifu hautawezekana.

Kifungu 86 cha Katiba kilibadilisha jinsi kura zinashughulikiwa zikihitaji kura kuhesabiwa, kuorodheshwa na matokeo kutangazwa na afisa anayesimamia kila kituo cha kupigia kura binafsi mara tu upigaji kura unapokamilika.

Kilitekelezwa kwa mara ya kwanza na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) 2013 na kilitumika katika chaguzi za 2017 na 2022.

Kiliimarishwa zaidi 2017 baada ya Korti ya Rufaa mnamo Juni 23, 2017 kutoa uamuzi kwamba matokeo yanayotangazwa katika vituo vya kupigia kura ni ya mwisho na hayawezi kubadilishwa na yeyote, ikiwemo mwenyekiti wa IEBC katika kituo cha kitaifa cha kujumlisha kura.

Hatua hiyo ilipokonya afisi ya kitaifa mamlaka ya kuthibitisha matokeo mashinani kwa namna inayoweza kubadilisha idadi, hivyo kufanya hesabu ya mashinani kuwa iliyo rasmi pekee.

Hakikisho la Bw Gachagua limejiri huku wasiwasi ukizidi kutanda kuhusu uadilifu wa chaguzi za 2027, kufuatia matamshi yaliyotolewa kuashiria njama za kuvuruga uchaguzi mkuu ujao kumpendelea.

Mazungumzo ya hivi punde kuhusu wizi wa kura yalizuka wikendi iliyopita wakati Naibu Gavana wa Kakamega, Ayub Savula na Mbunge wa Hamisi, Charles Gemose waliwaeleza bayana wajumbe wa UDA kutoka Magharibi kusaidia kuvuruga matokeo ya uchaguzi katika vituo vyao mtawalia vya kupigia kura siku ya uchaguzi.

Matamshi ya Bw Gachagua yamejiri saa chache baada ya Naibu Rais Kithure Kindiki kuwaonya viongozi wandani wa Rais Ruto dhidi ya kutoa madai kiholela kuhusu wizi wa kura, akisema bosi wake hahitaji kusaidiwa au kuvunja sheria ili ashinde kuchaguliwa tena.