Ruto anavyotongoza eneo la Magharibi akilenga 2027
JOTO la kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 linavyozidi kupanda, Rais William Ruto anaonekana kuweka matumaini makubwa ya kisiasa katika miradi miwili mikubwa ya miundombinu inayolenga eneo la magharibi mwa Kenya.
Miradi hiyo ni barabara kuu ya Rironi-Mau Summit yenye thamani ya Sh110 bilioni na upanuzi wa reli ya kisasa (SGR), kutoka Naivasha hadi Kisumu na Malaba unaokadiriwa kugharimu zaidi ya Sh500 bilioni.
Miradi hiyo inajiri wakati ambapo serikali ya Kenya Kwanza inakabiliwa na changamoto za kiuchumi, malalamiko ya wananchi kuhusu gharama ya maisha na mabadiliko ya kisiasa yanayoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa miradi hiyo si ya maendeleo pekee, bali pia ni uwekezaji wa kisiasa unaolenga kuimarisha uungwaji mkono wa Rais Ruto katika Bonde la Ufa, Magharibi na Nyanza kuelekea uchaguzi wa 2027.
Mchambuzi wa siasa, Bw Dismas Mokua, anasema umuhimu wa maeneo yanayofaidika na miradi hiyo hauwezi kupuuzwa.
Kwa mujibu wa takwimu za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) za uchaguzi wa 2022, eneo la Bonde la Ufa lilikuwa na zaidi ya wapigakura milioni 5.35, sawa na karibu asilimia 24 ya wapigakura wote nchini wakati huo.
Hii ndiyo ngome kuu ya kisiasa ya Rais Ruto na inatarajiwa kuwa muhimu katika juhudi zake za kutafuta muhula wa pili.
Zaidi ya Bonde la Ufa, miradi hiyo pia inaenea hadi Magharibi na Nyanza, maeneo ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakiegemea upande wa upinzani lakini sasa yanageuka kuwa viwanja muhimu vya kisiasa.
Kaunti nne za Magharibi mwa Kenya ambazo ni Kakamega, Bungoma, Busia na Vihiga zilikuwa na jumla ya wapigakura milioni 2.22 mwaka 2022.
Kwa upande mwingine, kaunti sita za Nyanza zilikuwa na zaidi ya wapigakura milioni 3.27.
Kwa pamoja, Bonde la Ufa, Magharibi na Nyanza zina karibu wapigakura milioni 10.84, idadi inayokaribia nusu ya wapigakura wote nchini.
Hii ndiyo sababu miradi ya barabara ya Rironi-Mau Summit na reli ya SGR imekuwa sehemu muhimu ya ujumbe wa kisiasa wa Rais Ruto kuelekea uchaguzi wa 2027.
Katika miezi ya hivi majuzi, viongozi wa upinzani wakiongozwa na Rigathi Gachagua na Kalonzo Musyoka wamekuwa wakifanya ziara za kisiasa katika eneo la Magharibi mwa Kenya wakijaribu kupunguza ushawishi wa Rais Ruto.
Hali hiyo imeongeza ushindani wa kisiasa katika eneo hilo.
“Rais na washirika wake wanaonekana kutaka kujibu hoja za upinzani kwa kuonyesha maendeleo yanayoonekana kupitia miradi mikubwa ya miundombinu,” anasema Bw Mokua.
Nguzo ya kwanza ya mkakati huo ni barabara ya Rironi-Mau Summit. Mradi huu ambao ulijadiliwa kwa miongo kadhaa bila kutekelezwa ulizinduliwa rasmi mwaka jana na Rais Ruto.
Barabara hiyo ya kilomita 139 kutoka Nairobi hadi Gilgil na Naivasha, inatekelezwa kupitia ushirikiano kati ya serikali na sekta ya kibinafsi. Inatarajiwa kubadilisha mojawapo ya njia muhimu zaidi za usafiri Afrika Mashariki.
Wakati wa uzinduzi wake, Rais Ruto alisema barabara hiyo si mradi wa usafiri pekee bali ni lango la ustawi, umoja na mabadiliko ya kiuchumi.
Alisema itarahisisha usafirishaji wa bidhaa na abiria, kuboresha usalama barabarani na kuimarisha nafasi ya Kenya kama kitovu cha biashara katika Afrika Mashariki na Kati.
Barabara hiyo inahudumia maeneo ya Kiambu, Nakuru, Baringo, Kericho, Nandi, Kakamega, Bungoma na Busia ambayo kwa pamoja yana mamilioni ya wapigakura.
Naibu Rais Kithure Kindiki pia ameendelea kuitangaza kama ushahidi wa uwezo wa serikali ya Kenya Kwanza kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo.
Akizungumza baada ya kukagua mradi huo wiki hii, Profesa Kindiki alisema barabara hiyo itamaliza msongamano wa magari na ajali nyingi ambazo zimekuwa zikishuhudiwa kwa miaka mingi katika njia hiyo.
Nguzo ya pili ya mkakati wa Rais Ruto ni upanuzi wa reli ya kisasa ya SGR kutoka Naivasha hadi Kisumu na Malaba.
Mradi huo ambao ulikwama kwa karibu miaka sita kutokana na changamoto za ufadhili, ulifufuliwa na serikali ya Kenya Kwanza na kuzinduliwa rasmi mapema mwaka huu.
Reli hiyo itapitia Narok, Bomet, Kericho, Kisumu, Siaya, Kakamega na Busia kabla ya kufika mpaka wa Uganda huko Malaba.
Maeneo mengi inayopitia reli hiyo kwa muda mrefu yamekuwa ngome za ODM.
Rais Ruto amesema reli hiyo itaweka Kenya katika nafasi bora ya kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Maziwa Makuu.
Pia alisema itafungua fursa za kiuchumi katika Magharibi mwa Kenya na kuunganisha maeneo ya uzalishaji wa kilimo na masoko ya ndani na nje ya nchi.
Wachambuzi wa siasa wanasema kuwa mbali na manufaa ya kiuchumi, mradi huo una uzito mkubwa wa kisiasa.
Kwa miaka mingi, baadhi ya wakazi wa Nyanza wamekuwa wakilalamikia kutengwa katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kitaifa.
Kiongozi wa ODM Oburu Oginga ameunga mkono mradi huo, akisema utaimarisha nafasi ya Kisumu kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika eneo la Ziwa Victoria.
Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi pia ametaja mradi huo kuwa muhimu kwa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Hata hivyo, mkakati wa Rais Ruto una changamoto zake.
Wakosoaji wake wanasema kuwa wananchi kwa sasa wanajali zaidi gharama ya maisha, ukosefu wa ajira na ushuru mkubwa kuliko miradi mikubwa ya ujenzi.
Pia kuna mashaka kuhusu iwapo miradi hiyo itakamilika kwa kiwango cha kuridhisha kabla ya uchaguzi wa 2027.