Afrika inavyoweza kuziba pengo la Dola 90 bilioni katika ufadhili wa kilimo
KWENYE ukumbi wa KICC, Nairobi ambapo mkutano wa Africa Forward Summit 2026 ulifanyika, viongozi kutoka sekta ya fedha, maendeleo na kilimo kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika walikutana kujadili changamoto moja kubwa inayokwamisha mageuzi ya kilimo barani — ukosefu wa fedha.
Miongoni mwa waliokuwa mstari wa mbele katika mjadala huo alikuwa Anny Caroll Bakang, Katibu Mkuu wa African Rural and Agricultural Credit Association (AFRACA). Kupitia Azimio la Nairobi lililowasilishwa wakati wa mkutano huo, taasisi za fedha za maendeleo barani Afrika, pamoja na washirika wenza waliweka wazi dhamira yao ya kuziba pengo la takriban Dola 90 bilioni, zinazokosekana kila mwaka katika ufadhili wa kilimo Afrika.
Kulingana na Bakang, suala hilo si takwimu tu. Ni maisha ya mamilioni ya wakulima wa mashamba madogo ambao wameendelea kuzalisha chakula licha ya changamoto za ukosefu wa mikopo, mabadiliko ya tabianchi na mifumo dhaifu ya kifedha.
“Wakulima wa mashamba madogo ndio uti wa mgongo wa usalama wa chakula Afrika, lakini wengi wao bado hawana uwezo kupata huduma za kifedha,” alisema.
Alieleza kuwa kwa karibu miaka 49, AFRACA imekuwa ikifanya kazi kuimarisha mifumo ya fedha mashambani na katika sekta ya kilimo. Kupitia Azimio la Nairobi, taasisi hiyo sasa inalenga kuhakikisha kuwa mjadala wa ufadhili wa kilimo unapiku zaidi ya sera na kuwa msaada wa moja kwa moja kwa wakulima. Isitoshe, malengo ya Azimio la Nairobi 2026, yananuwia kugeuza ahadi kuwa matendo kuboresha sekta ya kilimo kupitia ufadhili.

Kupitia ushirikiano na taasisi za maendeleo kama International Fund for Agricultural Development, ikiwa ni pamoja na French Development Agency, rasilimali zinatarajiwa kuelekezwa kwa taasisi za kifedha ambazo zitatoa mikopo na huduma nyingine kwa wakulima.
Bakang anasema ufadhili huo utahusisha mikopo ya muda mfupi, muda mrefu, pamoja na msaada wa kiufundi kwa taasisi za fedha ili ziweze kuelewa vyema mifumo ya uzalishaji wa kilimo.
“Kupata fedha pekee haitoshi. Taasisi za kifedha lazima zielewe kilimo na mahitaji halisi ya wakulima,” alisema. Kulingana na Katibu Mkuu huyo wa AFRACA, mojawapo ya matatizo makubwa ni kwamba taasisi nyingi za fedha bado zinaona kilimo kama sekta yenye hatari kubwa. “Sababu kuu ni kutofahamu jinsi sekta hiyo inavyofanya kazi.”
Kwenye mahojiano ya kipekee na Akilimali, alitoa mfano wa wakulima wa mahindi ambao wakati mwingine hulazimika kuanza kulipa mikopo hata kabla ya kuvuna mazao yao. Hali hiyo, alisema, huweka shinikizo kubwa kwa wakulima kwa sababu mfumo wa ulipaji hauenda sambamba na uhalisia wa uzalishaji wa kilimo.
Ndiyo maana AFRACA sasa inasukuma mifumo mipya ya kifedha kama warehouse receipt systems, ambapo wakulima wanaweza kuhifadhi mazao yao katika maghala yaliyoidhinishwa na kutumia stakabadhi hizo kupata mikopo.
Aidha, mfumo wa collateral registry unaruhusu wakulima kutumia mali kama mifugo au uzalishaji wa baadaye kama dhamana ya mkopo.
“Tumeona mifumo hiyo ikifanya kazi vizuri katika nchi kama Zimbabwe na Ghana,” alisema Bakang. Azimio la Nairobi pia linaegemezwa katika nguzo tatu kuu — kilimo himilivu na endelevu, ubunifu na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa Bakang, changamoto za ukame, mafuriko na misukosuko ya hali ya hewa zinaendelea kupunguza uzalishaji wa chakula Afrika, hivyo mifumo ya kifedha lazima iwe sehemu ya suluhisho.
Isitoshe, alisisitiza umuhimu wa value-chain financing, mfumo unaojumuisha wadau wote katika uzalishaji, usafirishaji, usindikaji na masoko ya mazao ili kurahisisha utoaji wa mikopo kwa wakulima.
Ingawa mataifa mengi ya Afrika yamewahi kusaini makubaliano ya Maazimio kama Malabo (2014), Maputo (2003) na Kampala yaliyotaka serikali kutenga angalau asilimia 10 ya bajeti kwa kilimo, Bakang anasema Azimio la Nairobi linatofautiana kwa sababu linaweka mkazo utekelezaji kwa njia ya vitendo.
“Hatutaki fedha zibaki katika mijadala ya sera na vyumba vya mikutano. Tunataka ziwafikie wakulima moja kwa moja,” alisema.
Kulingana naye, ushirikiano kati ya taasisi za fedha, serikali na washirika wa maendeleo ndio utakaoisaidia Afrika kufungua uwezo mkubwa uliopo katika sekta ya kilimo na kuimarisha usalama wa chakula kwa mamilioni ya watu barani.