Habari

Duale aepuka chawa wa jela, aonywa vikali asidharau mahakama

Na JOSEPH WANGUI, RICHARD MUNGUTI June 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KENYA imepima watu 104 waliokuwa wakishukiwa kuambukizwa virusi vya Ebola na kuwaweka karantini makumi ya wengine, wakiwemo baadhi ya maafisa wa serikali ya Rais William Ruto, Waziri wa Afya Aden Duale ameambia Mahakama Kuu.

Akijitetea kuhusu mpango tata wa kujenga kituo cha kutenga na kuhudumia wagonjwa wa Ebola katika Kituo cha Jeshi la Anga cha Laikipia, Bw Duale alisema nchi bado iko katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa huo kutokana na uhusiano wake wa karibu na mataifa ya Afrika Mashariki na Kati.

Siku moja baada ya kupatikana na hatia ya kudharau mahakama, Bw Duale aliomba radhi akisema hakuelewa ipasavyo maagizo ya mahakama yaliyositisha mradi huo unaoungwa mkono na Amerika.

Waziri wa Afya Aden Duale akiwa kortini na maafisa wengine wa wizara alikoshtakiwa kukiuka maagizo ya mahakama ya kusitisha ujenzi wa kituo cha karantini Nanyuki. Picha|Richard Munguti

Jaji Patricia Nyaundi alikubali ombi lake la msamaha, akakwepa kifungo cha jela lakini akaonywa vikali dhidi ya kukaidi amri za mahakama siku zijazo.

Mahakama ilikataa ombi la walalamishi waliotaka ahukumiwe kifungo cha miezi 15 gerezani na kulipa gharama za kesi hiyo binafsi.

Bw Duale alisema Wizara ya Afya imewapima watu 104 waliokuwa na dalili zinazofanana na Ebola, lakini hakuna aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa huo.

Visa hivyo vilirekodiwa katika kaunti za Nairobi, Uasin Gishu, Garissa, West Pokot, Bungoma, Kiambu, Busia, Kisumu, Nyeri, Kilifi, Nakuru, Nyamira, Wajir, Laikipia, Mombasa na Trans Nzoia.

Aliongeza kuwa zaidi ya wasafiri 139,000 wamechunguzwa katika mipaka ya kuingia nchini huku kaunti 25 zikitambuliwa kuwa katika hatari kubwa ya kuwa na visa vya Ebola.

Pia, alifichua kuwa zaidi ya Wakenya 40 walitengwa, wakiwemo wanachama wa ujumbe wa rais uliokuwa umetembelea Congo-Brazzaville.

Kwa mujibu wa Bw Duale, Rais Ruto alifuta safari ya kuhudhuria mkutano nchini Congo-Brazzaville baada ya kushauriwa na wataalamu wa afya na badala yake akashiriki kwa njia ya mtandao.