Siasa

ODM yafufua wito wa kutaka kushirikishwa kwenye fidia ya wahanga wa maandamano

Na JUSTUS OCHIENG June 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha ODM kimetaka kushirikishwa kikamilifu katika mchakato wa kuwafidia waathiriwa wa ukatili wa polisi na ukiukaji wa haki za binadamu uliotokea wakati wa maandamano kati ya mwaka 2017 na 2025.

Kupitia Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC), chama hicho kimesema kuwa ingawa kinaunga mkono mpango wa serikali wa kutoa fidia kwa waathiriwa, ni muhimu kihusishwe katika kubaini na kuthibitisha walengwa ili kuhakikisha haki na uwazi.

Katika azimio lake, ODM ilisema wengi wa waliouawa, kujeruhiwa au kupoteza mali wakati wa maandamano ya kisiasa walikuwa wafuasi wake, hivyo chama hicho kinafaa kuhusishwa moja kwa moja katika mchakato huo.

“ODM inafaa kushirikishwa kikamilifu ili kuhakikisha uwazi kwa kuwa ndicho chama kilichoathiriwa zaidi katika visa vingi,” chama hicho kilisema.

Kauli hiyo inajiri huku serikali ikitekeleza mpango wa Sh2 bilioni wa kufidia waathiriwa wa ukiukaji wa haki za binadamu uliohusishwa na maandamano na misukosuko ya kisiasa katika kipindi cha miaka minane iliyopita.

Mpango huo ulitokana na mapendekezo ya Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (NADCO) iliyoundwa baada ya mvutano wa kisiasa ulioshuhudiwa mwaka 2023.

Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga alipokutana na Profesa Makau Mutua na jopo la wataalamu wanaosimamia mpango huo, alisema hatua hiyo ni muhimu katika safari ya taifa kutafuta haki na maridhiano.

Dkt Oginga alisema Wakenya wengi wamekuwa waathiriwa wa ukatili wa polisi kwa miaka mingi bila kupata haki wala kutambuliwa.

Alitaja fidia iliyotolewa kwa mamake Baby Pendo kama mojawapo ya mafanikio ya kwanza ya mpango huo. Baby Pendo alifariki kufuatia operesheni ya polisi mjini Kisumu baada ya uchaguzi wa mwaka 2017.

Kwa upande wake, Prof Mutua alisema mpango huo ni wa kihistoria na unalenga kusaidia taifa kukabiliana na majeraha yaliyosababishwa na ukatili wa serikali kwa raia waliokuwa wakitekeleza haki zao za kikatiba.

“Hii ni fursa ya kipekee kwa taifa letu. Ni hatua ya kihistoria ambayo haijawahi kushuhudiwa,” alisema.

Alisisitiza kuwa fidia haimaanishi wale waliohusika na ukiukaji wa haki za binadamu wataepuka kuwajibishwa.

“Fidia haiwezi kuchukua nafasi ya uwajibikaji. Wale waliokiuka sheria lazima wawajibike,” alisema.

Kulingana na Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNCHR), jumla ya madai 1,937 yalipokelewa kutoka kwa waathiriwa wa visa vya kati ya mwaka 2017 na 2025, huku madai 1,101 tayari yakithibitishwa.

Rais William Ruto amesema serikali imetenga Sh2 bilioni kwa fidia hiyo, akisema ingawa fedha hizo haziwezi kurejesha maisha yaliyopotea, ni hatua muhimu ya kutambua maumivu ya waathiriwa na familia zao.