Pigo kwa chifu baada ya kuvuliwa wadhifa na korti kwa kuwa na alama ya D- KCSE
KILICHOONEKANA kuwa kilele cha safari ya utumishi kwa Lea Kalondu Ngutu katika utawala wa kitaifa, kiligeuka kuwa pigo baada ya mahakama kubatilisha uteuzi wake kuwa Chifu wa eneo la Mitaboni, Kaunti ya Machakos.
Mahakama ya Ajira na Leba mjini Machakos, ilitangaza uteuzi huo kuwa batili baada ya kubaini kuwa Bi Ngutu hakutimiza sifa za chini za kielimu zilizowekwa kwa nafasi hiyo.
Uamuzi huo ulitokana na kesi iliyowasilishwa na wakazi wawili wa Mitaboni, Stephen Nzomo Mutua na Anthony Ndonye Mutiso, waliopinga mchakato wa uajiri wa Wizara ya Usalama wa Ndani na Tume ya Utumishi wa Umma (PSC).
Kwa mujibu wa tangazo la kazi, waombaji walitakiwa kuwa na angalau alama ya C katika mtihani wa KCSE.
Hata hivyo, rekodi za mahakama zilionyesha kuwa Bi Ngutu alipata alama ya D-.
Licha ya kutotimiza kigezo hicho, aliorodheshwa, akahojiwa na hatimaye kuteuliwa kushikilia mojawapo ya nafasi muhimu zaidi katika utawala wa mashinani.
Walalamishi walidai kuwa mchakato huo ulikiuka kanuni za uwazi, usawa na ushindani wa haki katika ajira za umma.
Walisema waliotimiza masharti walinyimwa nafasi ya kushindania kazi hiyo kwa haki.Mahakamani, Bi Ngutu alitetea uteuzi wake akisema kuwa kufaulu kitaaluma hakupaswi kuwa kipimo pekee cha uwezo wa mtu kushikilia afisi ya umma.
Alieleza kuwa uzoefu wake kama Naibu Chifu ulimpa ujuzi wa kutosha wa kiutawala na ufahamu wa changamoto za eneo hilo.
Jaji aliamua kuwa uteuzi wa mtu ambaye hakufikia kiwango cha chini cha kielimu ulikiuka Kifungu cha 232(1)(g) cha Katiba kinachosisitiza ushindani wa haki katika ajira za umma.