Siasa

Magwanga amuonya Mbadi kwa kumpigia debe Wanga kwa Tutam

Na GEORGE ODIWUOR June 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Gavana wa Homa Bay, Oyugi Magwanga, amemtaka Waziri wa Fedha John Mbadi kuacha kuingilia siasa za Kaunti ya Homa Bay akisema hatua hiyo inaweza kuathiri haki ya wananchi kuchagua viongozi wanaowataka katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Kauli hiyo imejiri huku Bw Mbadi akiendelea kufanya ziara mara kwa mara katika maeneo mbalimbali ya Nyanza Kusini ambako amekuwa akieleza wananchi mipango ya serikali ya Rais William Ruto na kuhimiza uungwaji mkono wake kuelekea uchaguzi ujao.

Katika baadhi ya mikutano hiyo, Waziri huyo amekuwa akitoa kauli zinazotafsiriwa kuwa kujaribu kuelekeza wapigakura kuhusu viongozi wanaopaswa kuchaguliwa.

Akiwa katika eneo la Naytoto, Suba South mnamo Juni 7, Bw Mbadi alisema atawajulisha wananchi mgombea anayefaa kuungwa mkono katika eneo hilo wakati ufaao utakapowadia.

“Ni mimi ninayeamua nani anafaa kuchaguliwa Suba South. Nitawaeleza mgombea bora wakati ukifika,” alisema.

Bw Mbadi, ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Suba South kwa mihula mitatu kabla ya uchaguzi wa 2022, pia ameapa kuhakikisha mbunge wa sasa, Caroli Omondi, hapati muhula mwingine baada ya wawili hao kutofautiana kisiasa.

Aidha, katika ibada ya maombi iliyofanyika katika Kanisa la Seventh Day Adventist la Sombro mwishoni mwa wiki, Bw Mbadi aliwataka wakazi wa Homa Bay kumchagua tena Gavana Gladys Wanga mwaka 2027.

Alisema viongozi wakuu wa eneo hilo wameamua kuweka kando tofauti zao na kufanya kazi pamoja kuimarisha uungwaji mkono wa Rais Ruto huku akisisitiza kuwa haoni mgombea mwenye uwezo wa kumshinda Bi Wanga.

“Wengine wanaweza kuwania ugavana, lakini nina hakika tutawashinda,” alisema.

Kauli hizo hazikumpendeza Bw Magwanga ambaye anatarajiwa kuwania ugavana huo kwa mara ya tatu baada ya kushindwa katika uchaguzi wa 2017 na 2022.

Alisema Bw Mbadi anapaswa kujiepusha na siasa za kaunti kwa kuwa nafasi yake ya uwaziri inamtaka kuwa juu ya siasa za upande mmoja.

“Wananchi wa Homa Bay wana haki ya kuchagua gavana wanayemtaka bila kushinikizwa na viongozi wa kitaifa,” alisema.

Bw Magwanga pia alidai kuwa Bw Mbadi anaunga mkono kuchaguliwa tena kwa Bi Wanga kwa sababu za kibinafsi.

Kwa mujibu wake, gavana huyo anaweza kutafuta uteuzi katika Baraza la Mawaziri iwapo atapoteza kiti chake, jambo ambalo linaweza kuhatarisha nafasi ya Bw Mbadi serikalini.

“Tofauti za kisiasa hazipaswi kutumiwa kuwanyima wananchi haki yao ya kufanya maamuzi ya kidemokrasia,” alisema.

Wakati huo huo, tofauti kati ya Bi Wanga na Bw Magwanga zimeendelea kugawanya viongozi wa Homa Bay.

Baadhi ya madiwani wameanza kuonekana katika mikutano ya Bw Magwanga badala ya kuandamana na gavana huyo.

Bw Magwanga pia alikosoa utendakazi wa serikali ya kaunti akidai kuwa licha ya Homa Bay kupokea zaidi ya Sh36 bilioni kutoka wizara ya fedha, maendeleo yanayoonekana ni machache.

Alisema alijiuzulu kutoka wadhifa wa naibu gavana mwezi Februari kutokana na kile alichotaja kuwa kufadhaishwa na jinsi serikali ya kaunti ilivyokuwa ikiendeshwa.

Hata hivyo, licha ya tofauti zao za sasa, Bw Magwanga alisema yuko tayari kumuunga mkono Bw Mbadi iwapo atawania urais mwaka 2032.