Habari

Wimbi la utekaji nyara larejea nchini

Na KEVIN CHERUIYOT NA DANIEL OGETTA June 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KUIBUKA tena kwa visa vya watu kutoweka kwa njia tata kumezua hofu kuwa serikali inatumia njia hiyo kuwaandama wakosoaji wake.

Familia za Wakenya waliotoweka sasa zinaitaka serikali iwaachilie wapendwa wao wanaoamini walitekwa nyara kwa sababu ya kuukosoa utawala wa sasa.

Watu wanane wametoweka katika kipindi cha wiki moja iliyopita katika maeneo mbalimbali Nairobi, huku walioshuhudia wakisema walichukuliwa na wanaume wasiojulikana.

Kutoweka huko kumeongeza wasiwasi miongoni mwa mashirika ya kutetea haki za binadamu na familia kwamba visa vya kutekwa kwa lazima vinatumiwa kuwanyamazisha wakosoaji wa serikali.

Juhudi za familia za waliotoweka za kuwasaka katika vituo vya polisi, hospitali na mochari hazijafaulu.

Davies Lichuma, alihudhuria maandamano ya Juni 25 yaliyofanyika kuadhimisha mwaka wa pili tangu maandamano ya Gen Z ya 2024, lakini hakuwahi kurejea nyumbani.

Mamake, Margaret Lichuma, alisema alimshawishi mwanawe asiende kwenye maandamano hayo akihofia ukatili wa polisi na kutekwa nyara.

“Nilienda Kituo cha Polisi cha Central kuripoti tukio hilo baada ya kuambiwa katika Kituo cha Polisi cha Pangani kuwa waliokamatwa wakati wa maandamano walikuwa wamepelekwa Central. Lakini hadi sasa sijui alipo mwanangu Lichuma.

“Niliona waliokamatwa siku hiyo wakitupwa msituni baada ya kupigwa, lakini mwanangu sijamuona,” akasema mama huyo akiwa na huzuni.

Anaomboleza kifo cha binti yake ambaye bado hajazikwa, na sasa kutoweka kwa mwanawe kumeongeza majonzi katika familia hiyo.

Steven Mugo Miano na Beatrice Wanjira, wazazi wa Macmillan Kiarie, nao wanasema mwanao ametoweka tangu Juni 20 baada ya kudaiwa kutekwa nyara na watu wasiojulikana.

“Picha za CCTV zilionyesha kuwa alipotoka nyumbani saa tatu asubuhi Jumamosi, kulikuwa na gari lisilo na nambari za usajili lililokuwa limeegeshwa nje ya nyumba. Alivamiwa na kulazimishwa kuingia ndani ya gari hilo ambalo liliondoka kwa kasi. Hatujui alipelekwa wapi baadaye,” akjasema Bi Wanjira.

Kwa mujibu wa wazazi wake, Bw Kiarie amekuwa mstari wa mbele katika kuhamisha jamii kuhusu uongozi mbaya Mathare.

“Tumekuwa tukienda katika vituo vya polisi, lakini maafisa wamekuwa wakituzungusha wakisema lazima kwanza wapate simu ya Kiarie ili wachunguze watu aliokuwa akiwasiliana nao,” akasema mama yake.

Naye Michael Oloo, kwa mujibu wa rafiki yake Francis Ouma, alitekwa kutoka kinyozi katika eneo la Umoja 1.

Bw Ouma alisema alielezwa Bw Oloo alipigwa na kuingizwa kwa nguvu ndani ya gari lililoondoka kwa kasi. Tangu wakati huo hajulikani alipo.

“Tumemtafuta kila mahali, ikiwemo hospitali, mochari na vituo vya polisi, lakini hatujampata,” Bw Ouma akaambia Taifa Leo.

Pia Abdulaziz Duba Molu, maarufu kama Zizou hajulikani alipo.

Kwa mujibu wa kaka yake Ramadhan Duba Molu, alitoweka Juni 23 katika eneo la Juja Farm na hajaonekana tangu wakati huo.

“Aliondoka Kiamaiko kuelekea Juja ambako alikuwa amenunua kipande cha ardhi. Walipokuwa wakirejea nyumbani akiwa na marafiki zake, magari mawili yaliwazuia na wakaamriwa kulala chini,” akasema Bw Duba akirejelea maafisa waliokuwa wamevalia sare za polisi na wengine waliokuwa wamevalia kiraia huku wakiwa na silaha.

“Waliuliza Abdulaziz ni nani miongoni mwao, kisha wakamchukua na kuwaacha wengine,” akaongeza.