Habari

Ni uoga unawasumbua au?

Na MOSES NYAMORI NA COLLINS OMULO June 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MBUNGE wa Kiharu Ndindi Nyoro na baadhi ya wanasiasa wa ODM wamejipata katika hali ngumu kisiasa baada ya kushutumiwa kama viongozi vuguvugu ambao hawaegemei mrengo wa serikali ama upinzani.
Wanasiasa hao ni Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro, Otiende Amollo (Rarieda), Millie Odhiambo (Suba Kaskazini) Gavana wa Kisumu Profesa Anyang’ Nyongó, Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kisumu Ruth Odinga na Winnie Odinga, anayehudumu katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA).
Ikiwa imesalia miezi 13 kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027, wanasiasa hao wamekashifiwa kwa kushindwa kufanya uamuzi dhabiti na kutoa mwelekeo wa kisiasa kwa wafuasi wao.
Kutoamua mrengo walioko huenda kutasababisha wapoteze kura huku baadhi ya wafuasi wao wakianza kuwashutumu kwa usaliti na wengine kuwarejelea kama fuko.
Mnamo Jumamosi, Bw Nyoro aliomba apewe muda wa wiki tatu hadi nne kabla ya kutangaza mwelekeo wake wa kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027.
Wiki iliyopita alikumbana na ukosoaji mkali kutoka kwa umma baada ya kutoshiriki upigaji kura wa Mswada wa Fedha wa 2026.
Wakenya walimkejeli kwa kushindwa kufanya uamuzi licha ya kuwa kila mara yupo kwenye vyombo vya habari akikosoa serikali.
Katika mkutano wake na wanahabari Jumamosi, alikanusha kuwa na uhusiano wowote wa kisiasa na Rais Ruto. Bw Nyoro alikosana na Rais na baadaye akaondolewa katika wadhifa wa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Matumizi ya Bunge la Kitaifa.
Pia hajachangamkia pendekezo la kujiunga na mrengo wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambaye chama chake cha DCP kinaonekana kuwa na umaarufu mkubwa ukanda wa Mlima Kenya.
“Ni wazi kwamba niliondoka serikalini lakini naendelea kujibu swali hili si kwa sababu Wakenya wananiuliza, bali kwa sababu wanasiasa wanaendelea kunichokoza ili nilijibu,” akasema mbunge huyo.
“Mambo ambayo nimekuwa nikisema, hasa kuhusu uchumi, hayawezi kusemwa na mtu anayeiunga mkono serikali. Kama ungekuwa unaunga mkono serikali, ungewasilisha maoni yako ndani ya mfumo wa serikali,” akaongeza.
Dkt Amollo, Bi Odhiambo na Bi Ruth hawakuwapo wakati Bunge la Kitaifa lilipopiga kura kuhusu Mswada wa Fedha wa 2026.
Bi Ruth dadake marehemu Raila Odinga aliiambia Taifa Leo kuwa alikosa kufika bungeni kwa sababu alikuwa mgonjwa.
Wabunge hao watatu pamoja na Bi Winnie pia walikuwa miongoni mwa viongozi wakuu wa ODM ambao hawakuhudhuria mkutano mkubwa chama uliofanyika uwanja wa Kirembe Kisumu mnamo Mei 31.
Wiki iliyopita Bi Ruth alipuuza madai kwamba haegemei mrengo wowote akisema ataendelea kubaki ndani ya ODM.
“Ni bora tuwe na chama chenye nguvu, vinginevyo uwezo wetu wa kujadiliana utalemazwa . Nimetajwa kati ya walioshindwa kufanya maamuzi na kwamba nimeketi kwenye ua. Jinsi nilivyojibeba si ua hilo litaporomoka nikilikalia?” akasema katika hafla ya mazishi katika eneobunge la Nyando.
“Pia wanasema namdharau kaka yangu, Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga. Yeye ndiye kiongozi wa chama, ana uungwaji wangu na viongozi wengine,” akaongeza.
Hata hivyo, baadhi yao wamejitokeza hadharani kutetea misimamo yao ya kisiasa, wakisisitiza kuwa bado ni wanachama waaminifu wa ODM.
Dkt Otiende Amillo naye anasema alisalia ODM na kutojihusisha na mrengo wowote hakumaanishi alihama chama.
Mbunge huyo wa Rarieda anasema kuwepo kwa Linda Ground na Linda Mwananchi hakumaanishi kuwa ODM sasa imegawanyika
“Kuna watu walioondoka kwenye chama, wengine wakaenda kushoto na wengine kulia. Sisi tuliobaki pale chama kilipokuwa hatuwezi kuitwa watu ambao hawajaamua,” Dkt Amollo akaeleza Taifa Leo.
Pia amekuwa vuguvugu kuhusu uungwaji mkono kwa Rais Ruto akidai chama hakijawahi kuketi na kupitisha suala hilo kwa kauli moja.
“Wanaosema muhula mmoja au mihula miwili wanatoa maoni yao binafsi,” akasema.
Bi Winnie pia amekuwa akibadilisha msimamo kuhusu uungwaji wake mkono kwa Serikali Jumuishi.
Alipohudhuria Mkutano Maalumu wa Wajumbe wa ODM (SDC) Machi 27, alionekana kuunga mkono msimamo wa mjomba wake, Dkt Oginga.
Hata hivyo, tangu wakati huo ameonekana kubadili msimamo kwa kutohudhuria shughuli muhimu za chama. Mnamo Mei 15, wakati wa mazishi ya mama yake Seneta wa Kisii Richard Onyonka, alionekana kuunga mkono kambi ya Linda Mwananchi inayoongozwa na Edwin Sifuna.
Katika hafla hiyo aliwakosoa wanasiasa wanaoshirikiana na serikali ya Kenya Kwanza, akiwemo Waziri wa Fedha John Mbadi, kwa kuwataliki raia wa kawaida wanaolemewa na uchumi mgumu.