Wito serikali iimarishe msaada kwa wajane
WITO umetolewa kwa serikali, viongozi na watunga sera kuanzisha mipango endelevu ya kuwawezesha wajane.
Haya yanajiri huku wajane wengi nchini wakikabiliwa na umaskini, migogoro ya ardhi na jukumu la kulea watoto bila chanzo cha uhakika cha mapato.
Mary Khulisia, mmoja wa wajane katika eneo la Ikolomani alisema amepitia changamoto kadhaa tangu mume wake aage dunia.
“Unapata kuwa hata shamba lako unanyang’anywa kwa sababu huna mtu wa kukutetea. Tunahitaji kulindwa kama wajane,” aliambia Taifa Leo.
Mkurugenzi Mkuu wa International Center for Access to Justice (ICAJ), Wakili Laurine Magotsi, alisema hatua hizo zitasaidia kuboresha maisha ya maelfu ya wajane wanaopitia hali ngumu hasa baada ya kufiwa na waume wao.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wajane yaliyofanyika Ikolomani, Kaunti ya Kakamega, Magotsi alisema zaidi ya wajane 7,000 katika eneo hilo watanufaika na mpango wa shirika hilo unaolenga kuboresha upatikanaji wa haki, kuimarisha uchumi wao na kulinda mali walizoachiwa na waume wao.

Alisema ICAJ tayari imewapa wajane hao ofisi rasmi itakayotumika kwa mikutano, kuhifadhi kumbukumbu na kushughulikia masuala yao.
Magotsi alisema moja ya changamoto kubwa inayowakumba wajane ni migogoro ya ardhi baada ya vifo vya waume wao.
Alieleza kuwa wanawake wengi huishi katika mashamba yaliyotengwa kwa waume wao lakini umiliki haujawahi kuhamishwa rasmi, jambo linalowafanya wakwe au jamaa wengine kudai ardhi hiyo.
“Tulipokea karibu kesi 100 zinazohusiana na migogoro ya ardhi. Tutafanya ufuatiliaji wa kisheria ili kuwasaidia baadhi yao kupata hati miliki na kulinda haki zao za kumiliki mali,” alisema.
Aidha, alisema miradi ya kuwawezesha wajane kiuchumi lazima iwe endelevu, akisisitiza kuwa kuwapatia kuku au nguruwe pekee hakutoshi bila kuhakikisha wanapata chakula cha mifugo na usaidizi mwingine utakaowawezesha kupata mapato ya kudumu.
Pia aliunga mkono Mswada wa Kulinda Haki za Wajane unaofadhiliwa na Mbunge wa Rarieda, Otiende Amollo, akisema utasaidia kukomesha mila kandamizi na kuimarisha ulinzi wa haki za wajane nchini.