Gwiji Shisia Wasilwa anavyoendeleza Kiswahili kwa vipindi vya redio nchini na kimataifa
VYOMBO vya habari, ndani na nje ya Kenya hutekeleza dhima kuu katika makuzi, utetezi na usambazaji wa Kiswahili, ambayo ni lingua franca ya Afrika Mashariki.
Jukumu hili aghalabu hupigwa jeki maradufu pale ambapo wanahabari wanaofanya kazi katika taasisi hizo huwa ama ni wakereketwa wa Kiswahili au wana vipawa vya ajabu.
Katika kuviendeleza vipawa hivyo, huchangia kimakusudi katika kuendeleza na kunadi sera za Kiswahili.
Barani Afrika, Kenya, Tanzania, Zanzibar, Rwanda, Burundi, Uganda na Afrika Kusini hutoa huduma ya matangazo katika vituo vyao vya kitaifa vya redio.
Kuna vipindi vya Kiswahili katika vituo kama vile Kenya Broadcasting Corporation (KBC), Radio Tanzania, Dar es Salaam, Radio Rwanda, Kigali, Voice of Uganda, Kampala na Radio South Africa (R.S.A), Johannesburg.
Nje ya Afrika, kuna vituo kama vile British Broadcasting Cooperation – BBC, Sauti ya Ujerumani – Cologne (Radio Deutsche Welle), Radio Moscow (Urusi), Idhaa ya Kiswahili, Beijing, China, Voice of America (VoA), Radio India na vingine.
Mmoja wa wanahabari ambaye amepata fursa ya kufanya kazi katika kampuni za vyombo vya habari vya Kenya na vya kimataifa vinavyotumia Kiswahili ni Bw Shisia Wasilwa.
“Kwa zaidi ya miaka 20, nimejishughulisha na uandishi wa habari, uhariri na usimamiaji wa vipindi vya televisheni na redio katika mashirika ya habari ndani na nje ya Kenya,” anasema Bw Wasilwa.
“Mashirika ambayo nimewahi kuyafanyia kazi ni pamoja na KBC, Royal Media Services (RMS), Standard Media Group, China Radio Kimataifa, Deutsche Welle na BBC,” anasema Bw Wasilwa.
Baadhi ya vipindi vya Kiswahili alivyoandaa na kupeperusha hewani ni pamoja na ‘Ninapobanwa’ (RMS), ‘Jicho la Tatu’ (KTN) – ambacho kilikuwa sehemu ya kipindi maarufu cha ‘Nuru ya Lugha’.
Bw Wasilwa, aliyezaliwa Nakuru takriban miongo minne iliyopita anasema kuwa alivutiwa na sauti za watangazaji maarufu kuwahi kuibukia nchini kama vile Daniel Njuguna Gatei, Salim Mohamed (wote sasa ni marehemu) na Khadija Ali.
“Nilipokuwa mwanafunzi wa shule ya upili ya Bishop Delany – Uasin Gishu, nilianza kutunga mashairi na kushiriki kwenye public speaking nikiongozwa na walimu wangu kama vile Bi Khaemba Ongeti, Bw Oricho Omollo, miongoni mwa wengine,” anasema Bw Wasilwa.
Miaka mingi baadaye, kipawa chake cha utangazaji kiliimarika alipojiunga na KBC, baada ya kusomea stashahada ya uanahabari katika Taasisi ya Mawasiliano ya Kenya (KIMC) mapema miaka ya 2,000.
“Hapo nilipata kujifunza mengi kutoka kwa wanahabari wengine kama Martin Nyongesa King’asia, Mary Daraja, marehemu Leonard Mambo Mbotela, marehemu Khamis Themor, marehemu Destrrio Billy Omalla, marehemu Anaklet Araba, miongoni mwa wengine,” anasema.
Mbali na uanahabari, Bw Wasilwa pia ni mtunzi mahiri wa tungo za kiubunifu kwa Kiswahili.
Riwaya zake, mbali na kuidhinishwa na Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala ya Kenya (KICD) kusomwa katika mifumo ya elimu nchini Kenya, baadhi zimewahi kushinda tuzo za uandishi.
Kazi hizo ni: Dunia Tambara Bovu (EAEP, 2011), Makovu ya Uhai (Queenex, 2014) na Kengeza la Jasiri (African Ink 2022).
Makovu ya Uhai ilishinda Tuzo ya Fasihi ya Jomo Kenyatta mwaka 2022 na Mabati Safal Cornell Literature Prize mwaka 2018.
Aidha, Dunia Tambara Bovu ilitambuliwa na EAEP kuwa miongoni mwa kazi 20 bora kuwahi kuchapishwa na kampuni hiyo, katika utanzu wa riwaya.
“Katika taaluma yangu, nimewahi kuteuliwa mara mbili mtawalia kuwania Tuzo za Ubora Annual Journalism Excellence Award (AJEA) – katika kitengo cha Vipindi Bora vya Redio,” anasema Bw Wasilwa, ambaye kwa sasa ni Afisa wa Mawasiliano na Mauzo katika Chuo Kikuu Huria cha Kenya kilichoko Konza, Makueni.
“Vyombo vya habari vina wajibu na mstakabali maridhawa katika kukuza Kiswahili. Jukumu la kukiendeleza Kiswahili ni shughuli ya kikoa na kila mchango – hata uwe mdogo kiasi gani, utaongeza kani kubwa kwenye nguvu za kuvuvia tanuri ya ustawishaji wa Kiswahili,” anashauri Bw Wasilwa.