Lugha, Fasihi na Elimu

TALANTA: Chipukizi hodari wa kusoma habari kwenye runinga

Na RICHARD MAOSI June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

VALARY Wanjiku alipata motisha ya kusoma habari gwarideni baada ya kupata motisha kutoka kwa wanahabari nguli wa runinga pendwa ya NTV.

Akiwa mwanafunzi kutoka shule ya Msingi ya Multiple eneo la Kagio Kaunti ya Kirinyaga anasema usomaji wa habari humsaidia kujieleza mbele ya watu.

Siku za usoni analenga kuwa msomaji wa taarifa ya habari au msemaji wa mashirika makubwa nchini au Duniani.

Anasema ili kuwa msomaji mzuri wa taarifa ya habari mwanafunzi anatakiwa kuwa mkwasi wa lugha ya Kiswahili na Kiingereza.

Kwa upande mwingine anasema chama cha wanahabari katika shule yake hujumuisha wanafunzi wa madarasa yote.

Wamekuwa wakitumia talanta zao kusoma taarifa gwarideni Jumatatu na Ijumaa.

Aidha siku ya Jumatano wanahabari hutangamana ili kukusanya taarifa mbalimbali kutoka kwa wanafunzi wenzao kulingana na matukio ya wiki nzima.

Vilevile huongozwa na walimu wao namna ya kuripoti maswala ibuka yanayotokea katika jamii.

Valary huhakikisha anafanya mazoezi yake, kisha baadae hujitengea muda wa kuendelea na masomo yake ya kibinafsi.

Kwa upande wake anawamiminia sifa tele wazazi na walimu wake kwa kumhimiza kila mara asikate tamaa.

Vilevile shule yake imekuwa ikihakikisha wanafunzi wanapokea matini ya magazeti ya Taifa Leo na Daily Nation kila wiki ili kudondoa taarifa muhimu.

Anawashukuru walimu wake ambao wamekuwa wakihakikisha anapata fursa ya kuonyesha talanta yake siku ya wazazi shuleni na hata kwenye matamasha ya Muziki ya Kitaifa.

Kwa sauti yake nyororo anasema ili mwanafunzi awe mweledi katika usomaji wa taarifa ya habari ni lazima kuwa mpekuzi na mtafiti.

Uwezo wa kuchambua mambo kwa haraka, awe mkwasi wa lugha, jasiri na mwenye bidii.

Pia ashirikiane na wenzake kwa lengo la kupata habari za uketo kwa haraka na kadri zinavyotokea.