Fikirini aandikisha taarifa kwa polisi kuhusu mauaji ya mwanaharakati wa ODM
KATIBU wa Idara ya Masuala ya Vijana, Fikirini Jacobs, Alhamisi alifika katika makao makuu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Kanda ya Nairobi kutoa taarifa kuhusu uchunguzi wa kifo cha mwanaharakati wa vijana Cecil Ouma.
Bw Fikirini alisema aliitikia wito wa polisi ili kusaidia kubaini mazingira yaliyosababisha kifo cha Ouma, ambaye aliuawa kwa kupigwa risasi baada ya mkutano wa kuwawezesha vijana uliofanyika Kariokor na kuongozwa na Katibu huyo.
Akizungumza baada ya kurekodi taarifa yake, Bw Fikirini alisema yuko tayari kushirikiana kikamilifu na wachunguzi hadi ukweli ujulikane.
“Nitaendelea kujitokeza wakati wowote nitakapohitajika ili kusaidia uchunguzi kuhusu kifo hiki cha kusikitisha. Tunataka ukweli ujulikane na haki itendeke,” alisema.
Alisema kifo cha Ouma ni pigo kubwa kwa familia yake na jamii kwa ujumla, akisisitiza kuwa hakuna anayepaswa kupoteza maisha katika mazingira kama hayo.
“Nimefika hapa kutoa maelezo kuhusu yaliyotokea. Tayari watu saba, wakiwemo watatu kutoka ofisi yangu, wamehojiwa na kutoa taarifa zao,” aliongeza.
Ripoti za awali zinaonyesha kuwa Ouma alidaiwa kupigwa risasi na msaidizi anayehusishwa na Katibu huyo baada ya shughuli hiyo ya vijana kumalizika.
Kwa mujibu wa polisi, baada ya kupigwa risasi, Ouma alisukumwa kutoka kwenye gari akiwa amejeruhiwa.
Wakazi walimkimbiza katika Hospitali ya Park Road Nursing Home, lakini alifariki alipokuwa akipatiwa matibabu. Mwili wake ulihamishiwa katika Mochari ya Chiromo.
Maafisa wa upelelezi kutoka DCI wamesema watu saba tayari wametoa taarifa, wakiwemo walinzi wawili wa Bw Fikirini na mkurugenzi mmoja kutoka Wizara ya Masuala ya Vijana.
Inaelezwa kuwa mkurugenzi huyo alikuwa ndani ya gari moja na Katibu wakati tukio hilo lilipotokea.
Polisi pia wametwaa bunduki mbili zilizokuwa mikononi mwa walinzi wa Bw Fikirini ili zifanyiwe uchunguzi wa kisayansi kubaini ni ipi iliyotumika kufyatua risasi iliyomuua Ouma.
“Tumetwaa silaha hizo ili zifanyiwe uchunguzi wa kitaalamu kubaini ni bunduki gani iliyotumika,” alisema afisa mmoja wa upelelezi anayefahamu maendeleo ya uchunguzi.
Wakati huo huo, familia ya marehemu, marafiki na vijana wa Kariokor wanaendelea kusubiri matokeo ya uchunguzi wa maiti katika Mochari ya Chiromo huku wakitaka waliohusika na kifo hicho wawajibishwe.