Wabunge waendea Murkomen aeleze walipo vijana watatu waliotekwa nyara Kiamaiko
WABUNGE wanataka Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen kueleza walipo watu watatu wakazi wa eneobunge la Mathare waliopotea katika mazingira ya kutatanisha ndani ya kipindi cha saa 72.
Kutoweka kwa watu hao kulizua maandamano yaliyosababisha kifo cha mtu mmoja.
Mbunge wa Mathare Anthony Oluoch aliambia Bunge kuwa, watu hao ni Joel Kariuki Mwai, Michael Oloo Osura na Abdulaziz Molu, ambao familia zao zinaamini walikamatwa na maafisa wa usalama.
Bw Oluoch alisema Joel Kariuki Mwai, ambaye ni mfanyabiashara na aliwahi kuwania wadhifa wa MCA katika eneo la Mathare, alidaiwa kutekwa mnamo Juni 18, 2026, na watu waliokuwa wamevalia mavazi ya kiraia lakini walikuwa na silaha.
Siku iliyofuata, Michael Oloo Osura alitoweka katika eneo la Umoja karibu na Caltex.
Mnamo Juni 20, Maximilian Kiarie naye alidaiwa kukamatwa na watu waliokuwa wakitumia gari lisilo na nambari za usajili karibu na kituo cha Kizito, Githurai.
Siku hiyo hiyo, Abdulaziz Molu pia alitoweka katika eneo la Kiamaiko.
“Matukio haya yamezua hofu kubwa kwa familia zao kutokana na madai kwamba, walitekwa na watu waliojitambulisha kuwa maafisa wa usalama,” alisema Bw Oluoch.
Kutoweka kwa watu hao sasa ni miongoni mwa masuala ambayo Waziri Kipchumba Murkomen anatarajiwa kujibu mbele ya Bunge.
Wabunge wanataka waziri huyo aeleze walipo watu hao watatu na kubainisha iwapo kuna kitengo chochote cha usalama kilichohusika katika kukamatwa kwao.
Mbunge wa Starehe Amos Mwago alisema ongezeko la visa vya utekaji hasa jijini Nairobi limezua taharuki kubwa na kusababisha maandamano ambayo tayari yamesababisha kifo cha mtu mmoja Mathare.
“Tunataka Waziri atuambie walipo watu hawa ili kuzuia vifo zaidi kwa sababu wananchi bado wanaendelea kuandamana na wana hasira,” alisema Bw Mwago.
Bw Murkomen alitarajiwa kufika mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Utawala na Usalama wa Ndani Jumanne, lakini hakufika kwa sababu alihudhuria kikao cha Baraza la Mawaziri.
Badala yake, Katibu wa Idara ya Uhamiaji na Huduma za Raia Dkt Belio Kipsang aliwakilisha wizara hiyo na kuwaeleza wabunge kwamba Waziri alikuwa ameidhinisha rasmi amwakilishe.
“Jana jioni alinielekeza nihudhurie kikao hiki kwa niaba yake,” alisema Dkt Kipsang.
Hata hivyo, wabunge walikataa kuendelea na kikao hicho wakisisitiza kuwa masuala yaliyo mbele yao ni mazito na yanahitaji kujibiwa na Waziri mwenyewe.
Mwenyekiti wa kamati hiyo Gabriel Tongoyo alisema masuala hayo yanaweza kufafanuliwa ipasavyo na Waziri wa Usalama pekee.
Mbali na visa vya utekaji, wabunge pia wanataka Bw Murkomen afafanue madai kuhusu wageni wanaopata vitambulisho vya taifa na pasipoti za Kenya kwa njia isiyo halali.
Aidha, wanataka maelezo kuhusu hali ya usalama katika eneo la Angata Barikoi, Trans Mara, ongezeko la visa vya watoto kutoweka na mazingira ya kutatanisha yaliyosababisha kifo cha mtoto mmoja katika Kaunti ya Tharaka Nithi.
Wabunge wanataka kujua hatua ambazo serikali imeweka kuhakikisha uraia wa waombaji unathibitishwa kabla ya kupewa vitambulisho au pasipoti, pamoja na uchunguzi kuhusu wageni waliopata hati hizo kwa njia ya udanganyifu katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Mbunge wa Mount Elgon Fred Kapondi alisema Dkt Kipsang angeweza kujibu masuala yanayohusu uhamiaji pekee, lakini si yale yanayohusu usalama wa taifa.
“Iwapo Waziri alitaka kumtuma mwakilishi, basi alipaswa kumtuma Katibu wa Idara ya Usalama wa Ndani Dkt Raymond Omollo. Tunahitaji muda wa kumhoji Waziri mwenyewe kuhusu masuala haya nyeti,” alisema Bw Kapondi.
Naye Mwakilishi wa Wanawake wa Nakuru Liza Chelule alisema visa vya watoto kutoweka na ongezeko la ukatili wa kijinsia ni masuala ya dharura yanayohitaji majibu ya moja kwa moja kutoka kwa Waziri wa Usalama.
“Masuala haya ni mazito sana. Tunataka Waziri afike binafsi mbele ya kamati hii na kutoa majibu yatakayowatuliza Wakenya,” alisema Bi Chelule.