Sifuna: Mimi si mradi wa kigogo yeyote, tunachangisha pesa za mikutano kupitia Mpesa
KATIBU Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, amekanusha madai kwamba anafadhiliwa kisiasa na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ili kudhoofisha utawala wa Rais William Ruto huku uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027 ukikaribia.
Seneta huyo wa Nairobi, ambaye ameibuka kuwa kinara wa mrengo wa Linda Mwananchi ndani ya ODM, alitaja madai hayo kuwa propaganda za kisiasa akisisitiza kuwa shughuli za kisiasa za kundi hilo zinafadhiliwa na Wakenya wa kawaida pamoja na wafuasi wake, wala si vigogo wa kisiasa.
“Sifadhiliwi na Uhuru. Ninafadhiliwa na wananchi. Tuna tovuti ya umma na niko tayari kuonyesha taarifa za M-Pesa zinazoonyesha jinsi tunavyolipa DJ wetu na gharama za jukwaa,” alisema Bw Sifuna katika mahojiano na redio ya Egesa FM mnamo Jumatano, kuelekea mkutano wa kisiasa wa Linda Mwananchi unaopangwa kufanyika eneo la Gusii leo.
Aliongeza kuwa viongozi wa kundi hilo wanatumia rasilimali zao binafsi kufanikisha mikutano yao.
“Tuna magari yetu na sisi ni viongozi tuliochaguliwa na Mungu ametubariki. Huenda mimi si tajiri, lakini sitakosa mafuta ya kufika Kisii,” alisema.
Bw Sifuna alikuwa akijibu madai yanayotolewa na baadhi ya viongozi wanaounga mkono serikali jumuishi, hususan wanachama wa ODM wanaomuunga mkono Seneta Oburu Oginga, ambao wanadai kuwa shughuli za Linda Mwananchi zinafadhiliwa na Bw Kenyatta ili kuzua mgawanyiko ndani ya ODM na kuvuruga juhudi za Rais Ruto kutetea kiti chake mwaka 2027.
Hata hivyo, Seneta huyo alisisitiza kuwa hawategemei wafadhili wa kisiasa na kwamba wakosoaji wake wanaonyesha jinsi walivyozoea siasa za ufadhili na utoaji wa pesa kwa wafuasi.
“Siasa za kutoa hongo ndizo zinazofanya kampeni kuwa ghali. Sisi hatugawi pesa, wala fulana na kofia za kisiasa,” alisema.
Aliongeza kuwa wanasiasa waliozoea kufadhili mikutano yao kwa kugawa fedha hudhani kila kundi la kisiasa linaendeshwa kwa mtindo huo.
“Kama seneta, nina uwezo wa kuweka mafuta kwenye gari langu na kuhudhuria mikutano ya kisiasa popote nchini, sawa na viongozi wengine wa Linda Mwananchi,” alisema.
Bw Sifuna anatarajiwa kuongoza mkutano wa kwanza wa kisiasa wa vuguvugu hilo katika eneo la Gusii Ijumaa, baada ya mkutano uliokuwa umepangwa wiki iliyopita kuahirishwa ili kuwapa nafasi wafuasi kuomboleza waathiriwa wa maandamano ya vijana wa Gen Z ya Juni 25.
Mkutano huo ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya Linda Mwananchi inayolenga kufanya mikutano katika angalau kaunti 24 kabla ya kutoa tangazo kubwa la kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Miongoni mwa masuala yatakayojadiliwa ni iwapo vuguvugu hilo litaungana rasmi na muungano unaochipuka wa upinzani, na iwapo litamsimamisha mgombea wake wa urais au kujadiliana kuhusu mgombea mwenza katika muungano huo.
Viongozi wa Muungano wa Upinzani, akiwemo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, tayari wameeleza hadharani kuwa wako tayari kushirikiana na Linda Mwananchi ili kusimamisha mgombea mmoja wa upinzani dhidi ya Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Tangu kuanzishwa kwake, Linda Mwananchi limefanya mikutano ya kisiasa katika Dagoretti Kaskazini, Kitengela, Busia, Narok, Kakamega, Vihiga, Kisumu, Mombasa na Machakos.
Vuguvugu hili pia linapanga kufanya mikutano katika maeneo ya Mlima Kenya, ikiwemo Meru na Tharaka Nithi, kabla ya kuelekea Pwani katika kaunti za Kilifi na Kwale.
Ratiba yake pia inajumuisha mikutano ya kisiasa katika Eldoret, Siaya, Migori na Homa Bay, huku likilenga kupanua ushawishi wake kote nchini kabla ya uchaguzi mkuu ujao.