Mswada waundwa kubana maafisa wanaovujisha siri za serikali
MSWADA wapendekeza marufuku ya WhatsApp na barua pepe binafsi kwa shughuli za serikali
Maafisa wa umma huenda wakapigwa marufuku kutumia barua pepe binafsi au mitandao ya kijamii kama WhatsApp kusambaza nyaraka rasmi za serikali iwapo Mswada mpya uliowasilishwa bungeni utapitishwa kuwa sheria.
Mswada huo wa Marekebisho ya Sheria ya Upatikanaji wa Habari umedhaminiwa na Naibu Kiongozi wa Wengi Bungeni Owen Baya.
Unapendekeza kuwekwa kwa mfumo wa kisheria wa kulinda na kuainisha taarifa zinazomilikiwa na taasisi za serikali.
Kulingana na pendekezo hilo, afisa yeyote atakayevuja au kutumia vibaya taarifa za siri alizopata kazini, kuchapisha habari nyeti za serikali au kutumia barua pepe na nambari za simu zisizo rasmi kusambaza nyaraka za siri atatozwa faini ya hadi Sh1 milioni, kufungwa jela kwa hadi miezi sita au kupewa adhabu zote mbili.
Akizungumza mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Mawasiliano, Habari na Ubunifu, Bw Baya alisema mswada huo unapendekeza viwango vinne vya taarifa za siri, ambavyo ni siri kuu, siri, za siri za kawaida na zilizozuiliwa.
Alisema taarifa za kiwango cha juu zaidi zitakuwa zile ambazo zikivuja zinaweza kuhatarisha usalama wa taifa, usalama wa umma au maslahi ya Kenya.
Bw Baya alisema sheria ya sasa inatoa haki ya kupata habari chini ya Katiba, lakini haijaweka mwongozo wa kutosha kuhusu jinsi serikali inavyopaswa kulinda taarifa ambazo zinaweza kuhatarisha usalama wa taifa zikifichuliwa.
Aidha, mswada unapendekeza nyaraka zote za siri ziwekwe alama maalumu na zisajiliwe rasmi ili kuhakikisha uwajibikaji na kuzuia matumizi mabaya ya mfumo wa kuainisha taarifa.
Mbunge huyo wa Kilifi Kaskazini alisema aliamua kuwasilisha mswada huo baada ya kushuhudia maafisa wa sasa na wa zamani wa serikali wakisambaza nyaraka nyeti kupitia WhatsApp, X, televisheni na redio, licha ya kuapa kulinda siri za serikali.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mbunge wa Dagoretti Kusini John Kiarie, aliunga mkono pendekezo hilo akisema mashambulizi ya kimtandao dhidi ya mifumo ya serikali yanaongezeka. Alisema kamati yake inataka maafisa wote wa serikali watumie anwani rasmi za .go.ke pekee katika shughuli zote za kikazi ili kuimarisha usalama wa taarifa za serikali.