Matiang’i ajitetea baada ya kukutana na Arati na Junet
ALIYEKUWA Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Fred Matiang’i amelazimika kufafanua mkutano wake wa ghafla na Naibu Kiongozi wa Chama cha ODM Simba Arati pamoja na Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed, baada ya picha zao kusambazwa mitandaoni na kuzua mjadala mkali wa kisiasa.
Picha hizo zilionyesha viongozi hao wakizungumza katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA), jambo lililowafanya baadhi ya watu kudhani kulikuwa na mazungumzo ya kisiasa kati ya Matiang’i na viongozi wanaounga mkono serikali jumuishi.
Uvumi huo ulienea saa chache baada ya viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi kufanya mikutano ya kisiasa katika kaunti za Kisii na Nyamira, ambapo Matiang’i anahusishwa na upande wa upinzani.
Akijibu madai hayo, Dkt Matiang’i alisema hakukuwa na mkutano wowote wa kisiasa bali walikutana kwa bahati walipokuwa wakisafiri kuelekea Kisumu kwa shughuli tofauti.
“Asubuhi hii baada ya kuingia katika eneo la Kenya Airways katika Uwanja wa Ndege wa JKIA, nilikutana kwa bahati na Simba Arati pamoja na Junet Mohamed ambao pia walikuwa wakielekea Kisumu. Hakukuwa na mkutano wa kupanga wala mazungumzo ya kisiasa,” alisema Matiang’i.
Aliongeza kuwa baada ya hapo aliendelea na safari yake kuelekea Ahero kuhudhuria ibada katika Kanisa la SDA Apondo pamoja na Gavana wa Siaya James Orengo, kinara wa Narc Kenya Martha Karua na waumini wengine.
Junet pia alithibitisha kukutana na Matiang’i uwanjani humo, akisema kila mmoja alikuwa akielekea shughuli tofauti.
“Ni kweli tulikutana uwanja wa ndege. Mimi na Arati tulikuwa tunaelekea Nyando kwa shughuli ya kuwawezesha wananchi kiuchumi. Kama ilivyo kawaida kwa wanasiasa, tulizungumza kwa muda mfupi kisha kila mmoja akaendelea na safari yake,” alisema Junet.
Seneta wa Kisii, Richard Onyonka, aliwataka Wakenya kuacha kutoa tafsiri zisizo na msingi kuhusu picha hizo.
“Msifanye siasa za utoto. Matiang’i ndiye aliyepakia picha hiyo. Kukutana na viongozi uwanja wa ndege hakumaanishi umebadili msimamo wa kisiasa. Hata ningekutana na Rais William Ruto ningemsalimia na kupiga picha,” alisema Onyonka.
Wakati huo huo, mkutano wa Linda Mwananchi uliofanyika Gusii uligeuka kuwa wa lawama dhidi ya Gavana wa Kisii Simba Arati, ambaye viongozi wa mrengo huo walidai alihusika na kuvuruga mikutano yao.
Viongozi hao wakiongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi walidai magari yao yalipigwa mawe katika maeneo ya Keumbu na Nyaribari Chache na kwamba baadhi ya watu walijeruhiwa.
Walimshutumu Arati kwa kile walichodai ni kushirikiana na wapinzani wao wa kisiasa badala ya kusimama upande wa waliokuwa washirika wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga.
Katika mkutano huo, aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga alitangaza kuwa atashirikiana na mrengo wa Linda Mwananchi ili kuunganisha nguvu za upinzani kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Maraga alisema wananchi wanataka kurejeshewa nchi yao kwa kupambana na ufisadi na matumizi mabaya ya rasilimali za umma.
Siku mbili kabla ya tukio hilo, Kiranja wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Silvanus Osoro alimshauri Matiang’i kujiunga na upande wa serikali, akidai kuwa anaungwa mkono sana Kisii na nchini, huku akisema upinzani hauna nafasi ya kushinda uchaguzi wa 2027.