Habari

Jinamizi la kuamua mgombea mwenza wa Ruto 2027

Na JUSTUS OCHIENG July 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KINYANG’ANYIRO cha urais wa 2027 kimeanza kushika kasi, lakini nyuma ya pazia kuna pambano jingine lenye uzito mkubwa kumchagua mgombea mwenza.
Muungano wa Kenya Kwanza unaoongozwa na Rais William Ruto na muungano wa upinzani unaoundwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka na washirika wao, wote wanafanya hesabu za kupata mgombea atakayewaongezea nafasi ya ushindi.
Tofauti na chaguzi zilizopita ambapo nafasi ya mgombea mwenza ililenga zaidi kuvutia kura za eneo fulani, wakati huu hesabu ni tata zaidi. Zinachangiwa na mabadiliko ya miungano ya kisiasa, kuondolewa kwa Gachagua madarakani mwaka 2024, ushirikiano kati ya ODM na serikali ya Kenya Kwanza, mgawanyiko wa kisiasa katika eneo la Mlima Kenya na juhudi za upinzani kuunda muungano wenye uwezo wa kumng’oa Rais Ruto mamlakani.
Kwa upande wa Kenya Kwanza, Naibu Rais Kithure Kindiki bado anaonekana kuwa chaguo kuu la Rais Ruto.
Washirika wake wamekuwa wakisisitiza kuwa mwanasiasa huyo kutoka Tharaka Nithi ataendelea kuwa mgombea mwenza mwaka 2027. Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanaonya kuwa nafasi yake si ya uhakika kabisa.
Kutokana na hali hiyo, majina ya viongozi kadhaa yameendelea kutajwa kuwa huenda yakazingatiwa iwapo mazingira ya kisiasa yatabadilika. Miongoni mwao ni Mawaziri Wycliffe Oparanya na Hassan Joho, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, Magavana Anne Waiguru na Gladys Wanga pamoja na Waziri Mkuu wa zamani Musalia Mudavadi.
Kwa upande wa upinzani, hali ni ngumu vilevile. Ikiwa Kalonzo Musyoka atateuliwa kupeperusha bendera ya muungano huo, jina la Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna limekuwa likitajwa kama anayeweza kuwa mgombea mwenza. Vivyo hivyo, iwapo Fred Matiang’i hatapata tiketi ya urais, anaweza kuzingatiwa kwa nafasi hiyo.
Majina mengine yanayozungumziwa ni ya Martha Karua, Eugene Wamalwa, Justin Muturi na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya.
Kwa wachambuzi wa siasa, uteuzi wa mgombea mwenza ndio uamuzi mgumu zaidi kwa mgombea urais. Nafasi hiyo ni moja pekee, lakini lazima ikidhi matarajio ya kikanda, usawa wa kikabila, uimara wa muungano, uwezo wa kufadhili kampeni, tajriba ya uongozi, uaminifu wa kisiasa na hata mipango ya urithi wa uongozi.
Kwa sasa, wengi wanaamini Kindiki ndiye mgombea mwenye nguvu zaidi wa kuendelea kuwa naibu wa Rais Ruto. Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku amekuwa mstari wa mbele kutetea nafasi yake, akisisitiza kuwa hakuna nafasi ya mtu mwingine katika tiketi hiyo.
Rais Ruto pia ameonekana kuonyesha imani yake kwa Kindiki, hasa wakati wa ziara yake ya hivi majuzi katika Kaunti ya Meru. Tangu ateuliwe kuwa Naibu Rais, Kindiki amekuwa akifanya ziara za mara kwa mara katika eneo la Mlima Kenya, akizindua miradi ya maendeleo, kushiriki kuwawezesha wananchi kiuchumi na kuimarisha uhusiano na viongozi wa eneo hilo.
Hata hivyo, iwapo Rais Ruto atakubali kuwa hawezi tena kurejesha uungwaji mkono Mlima Kenya, huenda akalazimika kuelekeza nafasi ya mgombea mwenza katika eneo jingine ili kuongeza nafasi ya ushindi.
Hali hiyo imechangia kuibuka kwa majina ya viongozi wa ODM kama Wycliffe Oparanya na Gladys Wanga. Oparanya, aliyewahi kuwa gavana wa Kakamega na sasa Waziri wa Vyama vya Ushirika, anatajwa kuwa mwenye tajriba ya kuimarisha ajenda ya kiuchumi ya Rais Ruto.
Kwa upande wake, Wanga ameendelea kujijengea ushawishi wa kisiasa ndani ya ODM na kitaifa. Wafuasi wake wanaamini kuwa kumteua kunaweza kusaidia kuimarisha uhusiano kati ya Kenya Kwanza na ODM, kuongeza uungwaji mkono wa wanawake na kuvutia kura zaidi kutoka eneo la Nyanza.
Katika Pwani, viongozi wa kisiasa wameanza kampeni ya wazi wakitaka Waziri Hassan Joho apewe nafasi hiyo. Wanasema eneo hilo limekuwa likitoa mawaziri wenye ushawishi mkubwa lakini halijawahi kutoa Naibu Rais. Kwa mujibu wao, tajriba ya Joho katika siasa, uwezo wake wa kibiashara na mvuto wake kwa vijana vinamfanya kuwa mgombea anayefaa.
Magharibi mwa Kenya nayo imeendelea kutajwa katika hesabu hizo kupitia Musalia Mudavadi, ambaye bado anaheshimiwa kutokana na tajriba yake ya muda mrefu katika siasa za kitaifa. Wachambuzi wanaamini kuwa kumteua kunaweza kuimarisha nafasi ya Rais Ruto katika eneo hilo.
Kwa upande wa upinzani, Kalonzo Musyoka na Fred Matiang’i wameendelea kuonekana kama wagombea wakuu wa urais. Seneta wa Kitui Enoch Wambua hata alidai kuwa Gachagua ameamua kumuunga mkono Kalonzo kuwa mgombea wa urais wa muungano huo.
Kauli ya Kalonzo ilionekana kuthibitisha madai hayo aliposisitiza kuwa upinzani lazima uwe na mgombea mmoja dhidi ya Rais Ruto.
Hata hivyo, ziara ya kiongozi wa chama cha Safina Jimi Wanjigi nyumbani kwa Gachagua, Wamunyoro, ilibadilisha mwelekeo wa mjadala huo. Wanjigi anatajwa kuwa mmoja wa wanasiasa wachache wa upinzani wenye uwezo wa kugharimia kampeni ya kitaifa kwa fedha zake mwenyewe.
Aidha, iwapo Kalonzo atagombea urais huku Edwin Sifuna akiwa mgombea mwenza, eneo la Mlima Kenya halitakuwa na uwakilishi katika tiketi hiyo. Wachambuzi wanaona itakuwa vigumu kwa Gachagua kuwashawishi wapigakura wa Mlima Kenya kuunga mkono mpango huo. Hivyo, Wanjigi ameanza kutajwa kama chaguo mbadala kutoka eneo hilo.