Jinsi ya kulima maparachichi ya masoko ya ng’ambo
KILIMO cha maparachichi kimekuwa miongoni mwa biashara zenye faida kubwa nchini Kenya kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya matunda hayo katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
Masoko ya kimataifa, yaani ng’ambo, yamekuwa yenye mvuto mkubwa kwa maparachichi, maarufu kama avokado. Bara Uropa, nchi za Milki ya Kiarabu (UAE) na Asia ndio wanunuzi wakuu wa avokado za Kenya.
Ili kupata mavuno bora, mkulima anapaswa kuanza kwa kuchagua miche bora iliyothibitishwa kutoka kwa vitalu vinavyoaminika, anashauri Daniel Mwenda, mtaalamu.
“Aina maarufu zinazopendekezwa ni Hass na Fuerte kutokana na ubora wa matunda na soko lake,” Mwenda anasema.
Maparachichi hustawi katika maeneo yenye mvua ya wastani hadi nyingi, udongo wenye rutuba na usiotuamisha maji. Kabla ya kupanda, Mwenda anasema hatua ya kwanza ni kuandaa shimo lenye ukubwa wa karibu sentimita 60 kwa 60 na kuchanganya udongo wa juu na samadi ‘iliyooza’ vizuri. “Miche ipandwe kwa nafasi ya mita saba hadi nane kati ya mti na mti ili kutoa nafasi ya ukuaji,” anashauri mtaalamu huyo.

Miaka ya mwanzo, ni muhimu kumwagilia miche maji hasa wakati wa kiangazi, kuweka nyasi za matandazo (mulching) ili kuhifadhi unyevuunyevu na kupunguza magugu, pamoja na kuondoa matawi yaliyokauka au kuathirika na magonjwa.
John Mburu ni mkulima wa avokado Gatundu Kusini, Kaunti ya Kiambu na anasema amekumbatia matumizi ya mbolea asili na fatalaiza. “Mahitaji ya mbolea kwenye udongo, mkulima anapaswa kushirikisha mtaalamu ili upimwe kwenye maabara kujua virutubisho vinavyohitajika,” mkulima huyo anasema.
Wakulima wanapaswa pia kufuatilia wadudu na magonjwa, na kukabiliana na athari hizo kwa mujibu wa vigezo na dawa zilizoidhinishwa kwa minajili ya mazao yanayouzwa nje ya nchi.
“Matumizi ya mbinu bora za usimamizi wa mazao, ikiwemo usafi wa shamba na ushauri wa maafisa wa nyanjani, husaidia kupunguza hasara,” mtaalamu Mwenda anahimiza.

Mparachichi huanza kuzaa baada ya miaka miwili hadi mine – hilo likitegemea aina ya mche na usimamizi wa shamba. Matunda yanapaswa kuvunwa kwa uangalifu kwa kutumia vifaa vinavyofaa ili kuepuka majeraha yanayoweza kupunguza ubora wake.
Kwa wakulima wanaolenga soko la nje, ni muhimu kufuata viwango vya ubora kama GlobalG.A.P., kuhakikisha matunda yanachambuliwa vizuri na kuhifadhiwa katika mazingira yanayodumisha ubora wake.