Maoni

MAONI: Visa vya uhuni na ghasia za kisiasa vinaharibia sifa ya Kenya kimataifa

Na PAUL NABISWA July 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

YANAYOTUKIA Kenya wakati huu yanawatia wasiwasi wananchi na wenye nchi kwa sababu kadhaa.

Kwanza, wimbi kubwa la wahuni limechipuka mwaka mmoja kabla Kenya kuingia katika uchaguzi mkuu ujao wa Agosti 10, 2027.

Lawama zimeanza kurushwa huku na kule kuhusu mfadhili wa magenge haya, walengwa ni kina nani na mmiliki wa makundi haya anataka kuyafikia malengo gani?

Maeneo ya ibada si salama tena, wahuni wanaingia ndani na kuwahangaisha waumini.

Visa vilivyotokea huko Keumbu Kisii ambapo msafari wa Linda Mwananchi ulipovamiwa na kundi la vijana na kusabibisha kifo cha mtu mmoja lilikuwa jambo la kutisha.

Vivyo hivyo Jumapili iliyopita kulikuwa na kundi lililotaka kuvamia wafuasi wa Linda mwananchi waliokuwa katika kanisa la St Stephens Kisumu.

Baadhi ya vijana hao walikuwa na silaha hatari kama mishale na nyuta. Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna walikuwa kanisani humo kwa hafla ya mchango.

Kilomita kadhaa kutoka hapo katika Kaunti ya Nyandarua kundi jingine la Linda Mwananchi likiongozwa na Gavana wa Murang’a Irungu Kang’ata lilivamiwa likiwa jukwani.

Baadhi ya watu walijeruhiwa katika vurugu hizo.

Serikali imekanusha kuwa dereva wa Kang’ata alipigwa risasi ya mpira kifuani.

Kadhalika imesema kuwa haijapata rasmi taarifa kuhusu majeruhi katika fujo hizo.

Matukio haya pacha yameibua maswali mengi kuhusu usalama wa wanasiasa wakati huu ambapo baadhi yao wana makundi ya kuwalinda ambayo yako tayari kwa vita.

Kunapotukia vituko vya jinsi hii wafanyabiashara wengi wanafunga biashara zao ili wasipate hasara zaidi na wanaipata kwa sababu hawawahudumii wateja wao wakati huu.

Gavana wa Kisumu Prof Peter Anyang’ Nyong’o amewaonya vijana dhidi ya kutumiwa na wanasiasa.

Amezungumza kwa uchungu jinsi anavyokosa usingizi kuwatafuta wawekezaji ilhali vijana wameamua kuharibu biashara za watu.

Visa vingine vya ghasia vimeripotiwa katika eneo bunge la Ol Kalou ambapo uchaguzi mdogo unafanyika Alhamisi.

Vyama vya DCP na UDA ambavyo ndio washindani wakuu katika uchaguzi huo vimekuwa vikilaumiana.

Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua amelaumiwa na Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen kuwa anapanga kuleta fujo katika eneo bunge hilo.

Naye Gachagua amemkumbusha Murkomen kuwa ameshindwa kazi hivyo anatafuta vijisababu.

Vyombo vya usalama vina wajibu wa kukomesha msambao wa ghasia hizi.

Vinginevyo makundi mengi haramu yatajitokea kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027 na kuvuruga amani ya wahusika wote muhimu katika tukio hilo la kidemokrasia.

Matukio kama haya yanaweza kuchangia Kenya kutazamwa kwa jicho kali na mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu ICC.

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV