Mkenya afariki Amerika baada ya gari kutumbukia kwenye bwawa
WAKENYA wanaoishi Amerika wanaomboleza mauti ya Titus Wanjala, aliyefariki baada ya gari alilokuwa akiendesha kutumbukia kwenye bwawa mjini Waukee, jimbo la Iowa.
Wanjala, 43, pamoja na raia wa Amerika River Cropper, 23, wote wakazi wa Waukee, walifariki kufuatia ajali hiyo iliyotokea Julai 7.
Walioshuhudia tukio walisema gari hilo lilipoteza mwelekeo, likatoka barabarani na kutumbukia kwenye bwawa kabla ya vikosi vya kutoa msaada wa dharura kufika eneo hilo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Polisi ya Waukee, maafisa hao wa usalama walipokea habari saa 10 jioni saa za Amerika kuhusu gari lililokuwa limezama kwenye bwawa kando ya Barabara ya Manchester Boulevard, kati ya NW Charlestown Lane na NW Bennett Street.
Maafisa wa polisi na wazima moto walifika na kuanzisha juhudi za uokoaji. Walifanikiwa kuwatoa wawili hao majini lakini walifikishwa hospitalini wakiwa wameaga dunia.
Polisi wanaendelea kuchunguza chanzo cha ajali hiyo huku familia, marafiki na jamaa wakiendelea kuomboleza.
Mkuu wa Polisi wa Waukee, Chad McCluskey, alifariji familia za Wanjala na Cropper.
“Mioyo yetu iko pamoja na familia za Wanjala na River pamoja na wote walioathiriwa na msiba huu,” akasema.
Majirani wa wawili hao katika makazi ya Stratford Crossing Townhomes waliandaa sehemu maalumu ya kuwaenzi kwa kuweka maua na ujumbe wa rambirambi.
Mmoja wa majirani hao, Kaitlyn Cordero, alisema mwanzoni hawakujua kilichokuwa kimetokea.
“Tulipoona wakoaji wa dharura wakijitahidi kuwaondoa majini, ndipo tulitambua ukubwa wa ajali hiyo,” alisema.
Aidha, majirani hao waliandaa kesha na kuwasha mishumaa Jumapili ili kuwafariji wanafamilia na marafiki.
Mipango ya mazishi ya wawili hao inaendelea.