Askofu atimua mapadri saba kwa ukosefu wa nidhamu na mwenendo mbaya
JIMBO la Katoliki ya Maralal limewasimamisha kazi mapadri saba na kutangaza sheria kali zitakazodhibiti mwenendo, matumizi ya fedha na maisha ya kila siku ya makasisi.
Hatua hiyo imechukuliwa baada ya Askofu Hieronymus Emusugut Joya kusema kuwa tathmini ya kina aliyofanya ilibaini changamoto kubwa zilizokuwa zikikumba jimbo hilo.
Katika barua ya kichungaji ya kurasa nne aliyoandika Julai 12, askofu huyo alisema hatua hizo zimetokana na karibu miaka minne ya uchunguzi, ukaguzi wa hesabu na mashauriano tangu alipochukua uongozi wa dayosisi hiyo mnamo Oktoba 2022.
Askofu alisema alikuta jimbo hilo likikabiliwa na matatizo ya kifedha, kiutawala na kichungaji yaliyomlazimu kuanzisha mageuzi ya kurejesha uwajibikaji na nidhamu.
“Ni jambo la kuhuzunisha kusema kwamba nilikuta dayosisi hii ikiwa na matatizo mengi lakini hakuna aliyekuwa tayari kuniambia chanzo chake wala jinsi ya kuyatatua,” Askofu Joya aliandika katika barua hiyo iliyoripotiwa na shirika la habari za Kikatoliki la ACI Africa.
Alisema moja ya hatua zake za kwanza ilikuwa kuimarisha hali ya dayosisi kupitia michango na harambee huku akiweka mifumo mipya ya kuboresha utawala na usimamizi wa fedha.
“Hilo lilinisaidia kufanya tathmini ya dayosisi, kukagua hesabu za parokia zote, taasisi na ofisi, kuweka mifumo na miundo mipya, kufanya marekebisho na kulipa madeni pamoja na baadhi ya mikopo,” alisema.
Askofu huyo pia alitetea wito wake wa mara kwa mara wa kutafuta msaada wa kifedha akisema fedha zilizokusanywa zimebadilisha hali ya dayosisi.
“Nataka kila mtu ajue kwamba nimechangisha mamia ya mamilioni ya pesa tangu nifike hapa, zaidi ya kiasi ambacho waumini wote wa dayosisi hii wamechangia Kanisa lao kwa miaka mingi, bila hata kuhesabu miradi mikubwa iliyotekelezwa moja kwa moja katika parokia na taasisi mbalimbali,” alisema.
Askofu Joya alisema pia amekuwa akikosolewa kwa madai kwamba hakuwachukulia hatua mapadri waliotuhumiwa kuishi kinyume na wito wao wa kuhudumu au kumiliki mali ambayo chanzo chake hakikuweza kufafanuliwa.
Alisema alijizuia kuchukua hatua hadi alipokusanya ushahidi wa kuaminika.
“Sijawahi kumshuku wala kumwajibisha padri yeyote bila kuwa na taarifa za kuaminika. Kwa kuwa sasa nina taarifa hizo na nimewatambua mapadri husika, natangaza mambo mawili,” alisema.
Baadaye askofu alitangaza kuwasimamisha kazi mapadri saba na kuanzisha kanuni mpya za maadili kwa makasisi kwa mujibu wa Sheria za Kanisa.
Miongoni mwa masharti mapya, mapadri wote wanatakiwa kurejea katika vituo vyao kabla ya saa moja jioni kila siku kwa ajili ya sala za jioni.
Pia hawataruhusiwa kulala nje ya makazi yao bila idhini ya askofu. Maagizo hayo pia yanakataza watu wa kawaida kulala au kuishi katika nyumba za mapadri au nyumba za watawa bila kibali cha askofu.
Aidha, mapadri wamepigwa marufuku kunywa pombe katika baa au kuongoza Misa na ibada nyingine za Kanisa wakiwa wamelewa au wakiwa bado wanasumbuliwa na athari za ulevi.
Barua hiyo pia inawakataza mapadri kujihusisha na biashara binafsi nje ya kazi za Kanisa au kumiliki utajiri na mali ambayo hawawezi kueleza chanzo chake kwa njia ya kuridhisha.
Mageuzi hayo pia yanahusu usimamizi wa fedha katika dayosisi nzima.
Askofu Joya ameagiza parokia na taasisi zote za Kanisa kuimarisha kamati za fedha, kuandaa bajeti za kila mwaka, kufanyiwa ukaguzi wa hesabu mara kwa mara na kuhakikisha rasilimali za Kanisa zinasimamiwa kwa uwazi.
Pia ameweka masharti makali kuhusu matumizi ya magari ya dayosisi na kuwaagiza mapadri kutii kikamilifu sheria za Kanisa pamoja na sheria za Kenya.
Askofu alisema mageuzi hayo yanalenga kulinda heshima ya upadri, kuboresha usimamizi wa rasilimali za Kanisa na kurejesha imani ya waumini.
Katika barua hiyo ya kichungaji iliyoripotiwa kwanza na ACI Africa, askofu alisema hatua hizo za kinidhamu zilifuatia tathmini yake pamoja na kupokea taarifa alizozitaja kuwa za kuaminika kuhusu mwenendo wa baadhi ya mapadri na usimamizi wa mali ya Kanisa.