Dondoo

Mke wa pasta aomba vipusa ‘wapofuke’ wasione mumewe

Na KALUME KAZUNGU July 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

PASTA na waumini wa kanisa moja eneo hili waliachwa wakishangaa mkewe alipoporomosha ombi lisilo la kawaida.

Mama mchungaji huyo alikuwa ameambiwa na mumewe aombe ili kupisha kipindi cha maisha ya jamii.

Katika kuomba kwake, mke huyo wa pasta alisikika akimsihi Mola kuwafumba macho vipusa wote kanisani ili wasimuone na kumtamani mumewe.

Alifululiza kwa kumshukuru Mungu kwa kumpa mume mzuri na mtanashati. Pia alifichua jinsi amekuwa akishikilia roho mkononi kila anapoandamana na mumewe maeneo ya umma.

“Wajua vile ewe Mwenyezi Mungu umenipa mume mzuri, mtanashati. Pia hapa ukumbini najua kuna warembo wenye macho ya nje kama bwanangu. Basi ninakusihi kipindi hiki kinapoanza, wote hao wafunge macho, ikiwezekana wawe vipofu muda wote ili utukuzwe neno lako likipenya na kueleweka vizuri na hawa waja wako kabla uwarudishie macho yao,” akaendelea kuomba kwa unyenyekevu mwingi.

Ni hali iliyowaacha waumini na hata pasta mwenyewe wakishangaa hadi kufungua macho yao kwa kushangazwa na hata kutishwa na ombi hilo.