Habari

Digrii ya Didmus ya uhandisi ni feki, hakuwahi kuwa mwanafunzi wetu – Chuo cha JKUAT

Na MERCY SIMIYU September 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHUO Kikuu cha Jomo Kenyatta University of Agriculture and Technology (JKUAT) kimesema Mbunge wa Kimilili, Didmus Barasa, hakuwahi kuwa mwanafunzi chuoni humo wala hakikumtunuku shahada ya Uhandisi anayodai alihitimu mwaka 2008.

Katika barua aliyoandika Septemba 14, 2026, Msajili wa Masuala ya Kitaaluma wa JKUAT, Dkt Aggrey Wanyama, alisema jina la mbunge huyo halipo katika rekodi zozote za chuo hicho.

Chuo hicho pia kilipinga uhalali wa cheti kinachohusishwa na mbunge huyo, kikisema hakikufanya sherehe yoyote ya kuhitimu mwezi Mei 2008, tarehe iliyo kwenye cheti hicho.

“Jina lake halipo katika rekodi za wahitimu wetu, na JKUAT haikuwa na sherehe ya kuhitimu mwezi Mei 2008. Kwa hivyo, cheti chake cha Shahada ya Uhandisi wa Umeme na Elektroniki si halisi,” alisema Dkt Wanyama.

JKUAT ilieleza kuwa suala hilo liliwahi kuchunguzwa na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) pamoja na Bodi ya Wahandisi Kenya (EBK), na taasisi hizo zilipewa taarifa kuhusu uhalali wa sifa za kitaaluma zinazodaiwa na mbunge huyo.

Chuo hicho kilisema matokeo ya uchunguzi wake yalitumwa kwa EACC na EBK ili yashughulikiwe na hatua zinazostahili kuchukuliwa.

Hatua hiyo imefufua mjadala wa muda mrefu kuhusu historia ya elimu ya Barasa na vyeti ambavyo ametumia katika rekodi rasmi.

Kwa mujibu wa wasifu wa zamani uliokuwa kwenye tovuti ya Bunge la Kitaifa, Barasa alidai kusomea Shahada ya Sayansi katika Uhandisi wa Umeme na Elektroniki JKUAT kati ya mwaka 2001 na 2005.

Wasifu huo pia ulionyesha kuwa alisomea shahada ya uzamili nchini Australia.

Hata hivyo, wasifu wa sasa wa Bunge unaonyesha historia tofauti ya masomo.

Unaeleza kuwa alisomea Diploma ya Uhandisi wa Umeme na Elektroniki katika Chuo cha Mafunzo cha Kenya Power kati ya mwaka 2001 na 2004, kabla ya kupata Shahada ya Utawala wa Umma katika Chuo Kikuu cha Mount Kenya kati ya mwaka 2017 na 2021.

Aidha, wasifu huo unaonyesha alisomea Shahada ya Uzamili ya Utawala na Usimamizi wa Umma katika chuo hicho kati ya mwaka 2021 na 2022.

Mwaka huu, suala hilo lilirejea hadharani baada ya Shirikisho COFEK kuwasilisha kesi mahakamani likitaka kuthibitishwa kwa sifa za kitaaluma za mbunge huyo alipokuwa akijiandaa kuhitimu shahada ya uzamivu.

Barasa alitunukiwa Shahada ya Uzamivu katika Utawala wa Umma kutoka Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Murang’a mwezi Agosti 2026, huku maswali yakiendelea kuulizwa kuhusu vyeti vyake vya awali.

Katibu Mkuu wa COFEK, Stephen Mutoro, alisema taasisi za serikali zinapaswa kueleza hatua zilichukua baada ya kupewa taarifa na JKUAT.

“Ikiwa EBK ilikuwa na taarifa hizi, ni kwa nini mbunge anaendelea kutambuliwa rasmi kama mhandisi kitaaluma? Wakenya wanastahili kujua ukweli,” alisema.

Mbunge huyo hajatoa kauli rasmi kuhusu barua ya hivi punde kutoka JKUAT. Juhudi za kumtafuta ili kutoa maoni hazikufanikiwa.