Wakenya mpakani Tanzania wadumisha ushirikiano licha ya agizo tata lililohusu wageni
WAKAZI katika mipaka ya Kenya na Tanzania, maeneo ya Taveta na Lunga Lunga wamedumisha ushirikiano wao licha ya matukio ya hivi majuzi nchini yaliyotishia usalama wa wafanyabiashara wadogo ambao ni raia wa kigeni.
Kwa miongo mingi, raia wa nchi hizo mbili wamekuwa wakifanya biashara pamoja, kuoana, kuvuka mipaka kutafuta elimu bora, matibabu, na hata kushiriki pamoja kwa tamaduni zao.
Ushirikiano huo wa karibu ulijaribiwa kufuatia hatua za Kenya za kutekeleza kanuni za uhamiaji na biashara dhidi ya wafanyabiashara wa kigeni wasio na hati halali.
Wakati mjadala kuhusu wafanyabiashara wa kigeni ukiendelea kitaifa, shughuli za biashara katika maeneo mawili ya mpakani Pwani zinaendelea kwa kiasi kikubwa kama kawaida.
Wakazi wa Lunga Lunga, Kaunti ya Kwale, wanasema mpaka huo haujawahi kuwa kikwazo kikubwa kwa uwiano wao.
“Tunasoma na kuona kwenye vyombo vya habari kuhusu wageni wanaoondoka nchini, lakini katika eneo letu hatuwezi kuwabagua kwa sababu ni sehemu ya familia. Tunavua katika bahari moja, tumeoana na tunashiriki utamaduni mmoja,” alisema mkazi, Bw Juma Mwaguza.
Kulingana nao, mtu aliyezaliwa upande mmoja wa mpakani anaweza kuwa na ndugu, mwenzi wa ndoa au washirika wa biashara upande mwingine.
Familia huvuka mpaka mara kwa mara kwa ajili ya harusi, mazishi, shughuli za kidini, elimu na matibabu.
Vilevile, wakazi wanasema baadhi ya wafanyabiashara wa Tanzania hutumia marafiki au jamaa zao wanaoaminika nchini Kenya kupata huduma za pesa kwa njia ya simu na kusajili laini za simu, huku Wakenya wanaoishi karibu na mpaka wakiwa na mipango kama hiyo upande wa Tanzania.
Wanasema desturi hizo kwa kiasi kikubwa zinatokana na uaminifu uliojengwa kwa miongo mingi, wala si kwa nia ya kukwepa sheria za kitaifa.
Mpakani Taveta, utegemezi wa kiuchumi kwa Tanzania ni mkubwa zaidi hasa kwa bidhaa za kilimo.
“Jamii zimeungana na hatujaathiriwa na agizo hilo kwa sababu tunafanya biashara ya kuvuka mpaka. Lakini ikiwa agizo hilo litatulazimisha kubaki katika nchi zetu, Wakenya watateseka kwa sababu zaidi ya asilimia 60 ya bidhaa zinazouzwa katika soko la Taveta hutoka Tanzania,” alisema mfanyabiashara wa Tanzania, Bw Allen Kubo.
Soko la Kisasa la Taveta liko umbali wa takriban kilomita tatu pekee kutoka mpaka wa Kenya na Tanzania, hali inayowezesha mazao kuwafikia watumiaji haraka kupitia Kituo cha Pamoja cha Mpaka cha Taveta-Holili.
Wiki iliyopita, serikali iliwapa raia wa nchi za Afrika Mashariki wasio na hati halali nchini siku 90 kurekebisha stakabadhi zao za uhamiaji na kutimiza masharti ya leseni za biashara iwapo wangependa kuendelea kuendesha biashara nchini.
Agizo hilo lilizua wasiwasi miongoni mwa baadhi ya wafanyabiashara wa kigeni, huku mamia ya raia wa Burundi wakitafuta msaada katika ubalozi wao jijini Nairobi kutokana na hofu ya mashambulizi.
Nchini Uganda, gazeti la Daily Monitor liliripoti kuwa wafanyabiashara wa Uganda walikuwa miongoni mwa walioondoka Kenya wakihofia kushambuliwa.
“Taita Taveta ni kaunti yenye amani. Tunaishi pamoja na biashara zetu zinaendelea bila kikwazo chochote,” alisema Gavana Andrew Mwadime.
Jumuiya ya Afrika Mashariki inahimiza usafirishaji na uhamishaji wa watu, bidhaa na huduma miongoni mwa nchi wanachama, huku serikali za kila nchi zikipewa jukumu la kutekeleza kanuni za uhamiaji, ushuru na biashara.
Rais Ruto baadaye aliwahakikishia wawekezaji na wafanyabiashara wa kigeni kwamba Kenya bado iko wazi kwa biashara na uwekezaji.
Akizungumza wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi kwa hospitali inayojengwa na kampuni ya Tanzania, Dkt Ruto aliwaonya Wakenya dhidi ya kuwalenga raia wa kigeni wanaoendesha biashara ndogo nchini, akisema wako huru kufanya kazi nchini bora tu watii sheria za Kenya.