Akili Mali

Mashine hii mahuluti inafanya shughuli kibao shambani kuwa rahisi

Na SAMMY WAWERU July 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KILIMO cha usahihi [Precision Agriculture kwa Kimombo] kinaendelea kupata nguvu barani Afrika huku teknolojia zake za utekelezaji zikinuia kuwasaidia wakulima wadogo kuongeza kiwango cha uzalishaji mazao kwa kutumia mashine nyepesi na rahisi ila zenye uwezo mkubwa wa utendaji.

Moja ya teknolojia bunifu zilizovutia wakati wa makala ya 12 ya Maonyesho ya Teknolojia za Kilimo Afrika (Agritec Africa) wiki jana ni mashine inayoweza kufanya kazi anuwai za shambani.

Mashine hiyo Multipurpose Power Tiller imebuniwa na mjasiriamali barobaro kutoka India, Shubham Patel, ambaye ni mkurugenzi wa kampuni ya Alphachem yenye makao yake Gujarat.

“Mashine hii inampa mkulima uwezo wa kuendesha shughuli mbalimbali kwa kutumia kifaa kimoja badala ya kununua vingi tofauti,” Patel, 22, aliambia Akili Mali wakati wa maonyesho hayo yaliyofanyika Juni 17 hadi 19 katika jumba la mikutano la kimataifa la Kenyatta (KICC), Nairobi.

Mashine hiyo inaweza kutayarisha shamba, kulima, kupanda mbegu kwa kuzingatia nafasi na kina sahihi, kunyunyiza dawa ya kuua wadudu na magonjwa, kukatakata mimea ya malisho na hata kupiga maji kwa ajili ya unyunyizi.

Hali kadhalika, mtambo huu unaweza kuunganishwa kwa vifaa vya upanzi wa mimea kama mahindi, mtama, vitunguu, njugu na vitunguu.

Patel aeleza kuwa alitumia zaidi ya miaka mitatu na nusu kufanya utafiti na kuboresha mashine yake kabla kuizindua rasmi sokoni mwaka jana.

Anasema madhumuni yake yalikuwa kutengeneza mashine inayowezesha wakulima kufanya kazi kwa wakati unaofaa, jambo ambalo ni msingi wa kilimo cha usahihi.

“Wakulima wengi wadogo hawawezi kumudu gharama ya kununua au kukodi trekta na mashine kwa kila kazi. Mashine hii inawawezesha kufanya shughuli nyingi kwa kutumia kifaa kimoja na hivyo kupunguza gharama za uzalishaji,” asema.

Alihoji kwamba visa vya ucheleweshwaji wa shughuli za kilimo kama kulima, kupanda au kupalili hutokana pakubwa na wakulima kusubiri mashine za kukodi.

Power Tiller hii hutumia injini ya dizeli na inaweza kuchapa kazi katika ekari 10 hadi 15 kwa siku kutegemea shughuli inayotekelezwa.

“Pia imeundwa kwa vipuri vinavyopatikana kwa urahisi na mchakato wake wa utengenezaji ni wa kawaida tu,” alieleza Patel.

Kwa sasa Alphachem huunda karibu mashine 100 kila mwezi. Wakati wa maonyesho ya Agritec Africa 2026 mashine hiyo ilikuwa ikiuzwa kwa bei ya Sh420,000 ikiwa na vifaa vyake vyote.

Mkurugenzi huyo alisema licha ya bei hiyo kuonekana kubwa ni nafuu kuliko kununua mashine tofauti za kulima, kupanda, kunyunyizia dawa, kukata mimea ya malisho na kupiga maji.

Alidokeza kuwa wazo la kubuni mashine hiyyo lilitokana na ziara alizofanya katika nchi mbalimbali za Afrika.

Alibaini kuwa mashamba mengi yanaendelea kugawanywa kuwa madogo kutokana na urithi wa kifamilia, hali ambayo imefanya matumizi ya matrekta makubwa kutofaa kwa wakulima wengi wa mashamba madogo.

“Kilimo cha usahihi kinahitaji mashine zinazoendana na saizi ya shamba na zinazoweza kutekeleza kazi kwa urahisi na ufanisi pasipo kuongezea mkulima gharama,” akaongeza.

Waziri wa Kilimo na Mifugo Mutahi Kagwe, ambaye alifungua rasmi maonyesho hayo, alihimiza wakulima kukumbatia teknolojia na mashine za kisasa ili kuongeza uzalishaji wa mazao na mapato, jambo ambalo pia litavutia vijana kuingia kwenye sekta ya kilimo kama biashara.

“Mashine za bei nafuu zinaweza kununuliwa au kukodishwa na vyama vya ushirika au makundi ya wakulima, na hivyo kurahisisha upatikanaji wa huduma za kisasa za kilimo,” Kagwe alisema.

Mbali na mashine hiyo Alphachem pia huuza pampu za kupiga maji, mashine za kukatakata malisho na vifaa vya kupanda mbegu katika nchi mbalimbali za Afrika ikiwemo Kenya, Uganda, Tanzania, Zambia, Ghana, Angola, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DR Congo).