Ugatuzi: Kilichozima kabisa jumuiya za kiuchumi za kaunti
MIAKA 13 baada ya ugatuzi kuanza, ndoto ya kuanzishwa kwa jumuiya za kiuchumi za kaunti ili kuimarisha maendeleo imekwama kutokana na ukosefu wa fedha, mvutano wa kisiasa na kukosekana kwa sheria zinazozitambua rasmi.
Magavana walipoanzisha ushirikiano huo mwaka wa 2013, waliahidi kwamba ungechochea ukuaji wa uchumi, kuvutia wawekezaji na kuboresha maisha ya wakazi kupitia miradi ya pamoja.
Kaunti mbalimbali ziliunda miungano kama Jumuiya ya Kaunti za Pwani, Jumuiya ya Kiuchumi ya kaunti za eneo la Ziwa (LREB), Jumuiya ya Kiuchumi ya Kaskazini mwa Bonde la Ufa (Noreb), Jumuiya ya Kiuchumi ya Eneo la Kati(Cereb), Jumuiya ya Kiuchumi ya Kusini Mashariki Kenya na na Baraza la Ustawi la Kaunti za Kaskazini Mashariki.
Hata hivyo, matumaini hayo yamefifia. Miradi mingi imekwama huku baadhi ya kanda zikigeuka kuwa majukwaa ya mikutano bila matokeo yanayoonekana.
Baadhi ya changamoto zinazotajwa ni ukosefu wa fedha, ushindani wa kisiasa, mabadiliko ya uongozi wa kaunti na kukosekana kwa sheria inayoruhusu kaunti kuchangisha na kutumia fedha kwa pamoja.
Mfano ni LREB, iliyopanga kuanzisha benki ya maendeleo ya Sh2 bilioni ili kutoa mikopo nafuu kwa wafanyabiashara.
Mpango huo ulisitishwa mwaka wa 2023 baada ya Afisi ya Mdhibiti wa Bajeti kukataa kuidhinisha mradi huo kwa sababu haukuwa na msingi wa kisheria.
Kila kaunti mwanachama ilitarajiwa kuchangia Sh200 milioni, lakini hilo halikufanyika.
Mkurugenzi wa Kamati na Mipango katika Baraza la Magavana (CoG), Bw Kizito Osore Wangalwa, amesema ukosefu wa sheria ndio kikwazo kikubwa.
Alisema sheria itapatia kanda hizo uhalali, kurahisisha upatikanaji wa fedha kutoka kwa washirika wa maendeleo na kuhakikisha zinaendelea hata baada ya mabadiliko ya kisiasa.
Mswada wa Rasilmali za Kaunti unaolenga kutambua rasmi kanda hizo na kuruhusu kaunti kuunganisha rasilimali, bado umekwama Seneti.
Wataalamu wa utawala pia wanasema kuchelewa kwa sheria hiyo kumedhoofisha utekelezaji wa miradi mingi.
Mtaalamu wa utawala Dkt Peter Mbae alisema mabunge mengi ya kaunti hayajapitisha sheria zinazowezesha matumizi ya fedha kwa shughuli za kanda hizo, hali inayozua maswali ya ukaguzi wa hesabu.
Katika Jumuiya ya Kaunti za Pwani, mwenyekiti wake ambaye pia ni Gavana wa Tana River, Dhado Godana, amesema baadhi ya kaunti hazijawasilisha michango yao ya kila mwaka ya Sh2.5 milioni, jambo linalotatiza shughuli.
Licha ya changamoto hizo, wataalamu wanaamini kuwa ikiwa zitawekewa msingi wa kisheria na kufadhiliwa ipasavyo, miungano ya kiuchumi ya kanda inaweza kuimarisha kilimo, utalii, biashara, viwanda na kuongeza ajira kupitia miradi ya pamoja inayovuka mipaka ya kaunti.