Habari za Kitaifa

Magenge ya ulanguzi wa bangi yazidisha ujanja kuificha kwa ndizi, biskuti kuhepa polisi

Na VITALIS KIMUTAI August 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MISAKO mikali ya Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) dhidi ya dawa za kulevya katika kipindi cha miezi sita iliyopita imefichua mbinu mpya zinazotumiwa na walanguzi kusafirisha na kusambaza bangi nchini wakikwepa mtego wa polisi.

Uchunguzi umebaini kuwa walanguzi wamebadili njia za usafirishaji, aina ya magari wanayotumia na hata mbinu za kuficha mzigo ili usigunduliwe.

Baadhi yao sasa hupanda bangi katikati ya mashamba ya mahindi na mazao mengine ili kuficha mimea hiyo.

Baada ya kuvunwa, huifunga kwa ustadi na wakati mwingine kuificha ndani ya bidhaa kama vile ndizi, biskuti au marobota ya nguo kabla ya kuisafirisha.

Aidha, badala ya kutumia malori makubwa, sasa wanatumia magari madogo ya kibinafsi kama Toyota Probox na Toyota Wish, ambayo hayushukiwi kwa urahisi.

Kutoka mpakani Sirare, bangi husafirishwa kwa pikipiki ikiwa imefichwa kama mizigo ya kawaida kabla ya kukabidhiwa kwa mawakala wanaoipakia upya kwenye magari yanayoelekea Nairobi na miji mingine.

Mashambani

Walanguzi pia hutumia barabara za mashambani zisizo na vizuizi vya polisi, hasa usiku, alfajiri au jioni, ili kukwepa ukaguzi.

Wakati mwingine bangi husafirishwa kwa mabasi na matatu ikiwa imefichwa pamoja na mizigo halali katika hifadhi za mizigo.

Katika visa vingine, maafisa wa DCI wamekuta bangi ikiwa imefichwa ndani ya magunia ya ndizi, marobota yaliyofungwa kwa karatasi maalumu na hata masanduku ya chuma.

Mkurugenzi wa DCI Mohamed Amin alisema magenge ya kisasa ya dawa za kulevya sasa yanafanya kazi kama mitandao ya kimataifa inayotumia teknolojia na mbinu mpya za usafirishaji.

“Ufanisi wa vita dhidi ya dawa za kulevya haupimwi kwa idadi ya waliokamatwa bali kwa ubora wa uchunguzi, kufanikiwa kwa mashtaka na kuvunjwa kabisa kwa mitandao ya uhalifu,” akasema.

Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen naye alisema serikali itaendelea kuimarisha operesheni za kijasusi ili kuwafuatilia walanguzi na kuvunja mitandao yao.

Katika miezi ya hivi karibuni, DCI imekamata shehena kadhaa za bangi zenye thamani ya mamilioni ya pesa katika maeneo mbalimbali nchini, huku ikiwataka wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kukomesha biashara hiyo haramu inayozidi kuhatarisha jamii, hasa vijana na wanafunzi.