Wakora sasa watawala kituo cha mabasi cha Green Park Terminus kilichogharimu Sh250 milioni
UCHUNGUZI umeibua madai kuwa Kituo cha mabasi cha Green Park jijini Nairobi, kilichojengwa kwa gharama ya Sh250 milioni ili kupunguza msongamano wa magari katikati mwa jiji, kinadhibitiwa na vijana wanaodaiwa kuwa na uhusiano na viongozi wakuu wa Serikali ya Kaunti ya Nairobi.
Duru kutoka City Hall zinadai kuwa vijana hao hukusanya ada za maegesho kutoka kwa mabasi na magari huku maafisa rasmi wa kaunti wakitengwa.

Inadaiwa kuwa fedha zinazokusanywa haziingii kwenye hazina ya kaunti.
Ingawa hivyo, Afisa Mkuu wa Idara ya Mapato Tiras Njoroge, alikanusha madai hayo akisema kituo hicho kinaendelea kuingiza mapato, lakini hakutoa ushahidi.
Uchunguzi pia ulibaini kuwa kituo hicho kiko katika hali mbaya, huku baadhi ya huduma zikiwa hazifanyi kazi.

Aidha, kaunti imeidhinisha ujenzi wa kituo cha mafuta na inapanga kukodisha sehemu ya eneo hilo kwa kampuni ya China kujenga kituo cha kupasha moto magari ya umeme.
Awali, Green Park ilikusudiwa kuwa kituo cha kushusha na kuwachukua abiria wa mabasi ya masafa marefu na matatu, lakini haijatimiza lengo hilo tangu ilipokamilika.