Habari

Afisa wa polisi aliyemuandama barabarani na kumpiga risasi Dkt Mutiso afikishwa kortini

Na RICHARD MUNGUTI August 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AFISA wa polisi anayetuhumiwa alimpiga risasi Dkt Victoria Mutiso siku 13 zilizopita alifikishwa kortini Jumatatu (Agosti 10, 2026).

Konstebo Elijah Kibelion Kimoi kutoka kituo cha Polisi cha Karinde kilichoko eneo la Kikuyu alifikishwa mbele ya hakimu mwandamizi mahakama ya Milimani Paul Mutai.

Konst Kimoi alifikishwa kortini pamoja na Daniel Mwangi Njoroge na Kevin Ngugi Kinuthia.

Akiomba washukiwa hao wazuiliwe kwa siku 30, Koplo Romana Oduor anayechunguza kesi hiyo alisema Njoroge ndiye alikuwa anaendesha gari lililomzuilia Dkt Mutiso kabla ya kutwangwa risasi kichwani na Konst Kimoi.

Washukiwa wa mauaji ya Dkt Victoria Mutiso, Elijah Kimoi (kulia), Daniel Mwangi Njoroge na Kevin Ngugi Kinuthia walipofikishwa kortini Agosti 10, 2026. Picha|Richard Munguti

Mahakama ilielezwa Kinuthia ni mwendesha piki piki iliyompeleka Konst Kimoi kumuua Dkt Mutiso.

Baada ya kukamilisha zoezi la kumwangamiza daktari huyo wa tiba ya ubongo, Kinuthia alimhepesha Konst Kimoi.

Hakimu alielezwa kuwa baada ya mwili wa Dkt Mutiso kufanyiwa upasuaji kulitolewa risasi iliyofanyiwa utafiti na kubainika ilifyatuliwa kutoka kwa Bastola aina ya Mini Jericho iliyokuwa imepewa afisa mkuu wa polisi ambaye ametoroka.

Dkt Mutiso aliuawa kinyama mnamo  Julai 29, 2026.

Mahakama iliombwa iwazuilie washukiwa hao watatu kwa siku 30 kusaidia polisi kukamilisha zoezi la uchunguzi kubaini kilichopelekea daktari huyo kuuawa.

Mahakama ilielezwa mbali na watatu hao, kuna washukiwa wengine wanne waliotiwa nguvuni wiki mbili zilizopita kufuatia mauaji hao.

Wengine wanaozuliwa ni pamoja Rose Mbithe Mulwa na watoto wake Chris na Angella ambao ni mawakili.

Bi Mulwa alikuwa mke wa Prof David Musyimi Ndetei aliyetalikiwa na ambaye alikuwa anamenyana na Dkt Mutiso kuhusu umiliki wa ardhi ya ekari 20 iliyoko Mlolongo, Athi River, Kaunti ya Machakos.

Mwingine ni Nelson Masiga.

Washukiwa wa mauaji ya Dkt Victoria Mutiso wakiwa kortini Agosti 10, 2026. Picha|Richard Munguti

Mahakama ilifahamishwa polisi wanajaribu kung’amua kitendawili iwapo huenda mzozo wa shamba hilo la Mlolongo ulichangia kuuawa kwa Dkt Mutiso aliyezikwa kijiji cha Wanzauni, Kaunti ya Makueni Agosti 8, 2026.

Kesi ya mzozo huo wa shamba inaendelea katika mahakama kuu Machakos.

Konst Kimoi na wenzake wawili watarudishwa kortini Septemba 30, 2026 nao Bi Mulwa na watoto wake watafikishwa kortini Agosti 18, 2026 polisi kueleza ikiwa wamekamilisha ushahidi kubaini mchango wao katika mauaji ya mkurugenzi huyo wa kituo cha utafiti cha tiba ya maradhi ya akili.

Angella na Masiga waliagizwa na mahakama ya Mavoko wazuiliwe kwa siku 14 wahojiwe ikiwa walighushi hatimiliki ya shamba hilo lililoko Mlolongo.