Gavana ahepa makao makuu ya thamani ya Sh740 milioni
JENGO la makao makuu ya Serikali ya Kaunti ya Turkana lililogharimu zaidi ya Sh740 milioni na kuchukua zaidi ya miaka 11 kukamilika bado halijatumika kikamilifu, mwaka mmoja baada ya kukabidhiwa rasmi kwa serikali ya kaunti.
Jengo hilo la ghorofa nne lililoko Lodwar lilikabidhiwa serikali ya kaunti Julai 28, 2025, baada ya Seneti kuingilia kati kuharakisha ujenzi wake.
Hata hivyo, Gavana Jeremiah Lomorukai na idara nyingi za kaunti bado hawajahamia jengo hilo, hali inayozua maswali kuhusu matumizi ya fedha za umma zilizowekezwa katika mradi huo.
Ujenzi ulianza mwaka 2015 chini ya gavana wa kwanza wa Turkana, Josphat Nanok. Gharama ya mradi huo ilipanda kutoka Sh695 milioni hadi karibu Sh1.2 bilioni kutokana na mabadiliko ya usanifu na kazi zilizoongezwa.
Akizungumza mbele ya Kamati ya Seneti kuhusu Ugatuzi, Gavana Lomorukai alisema kaunti tayari imelipa Sh740.7 milioni huku kiasi cha takriban Sh24 milioni pekee kikisalia kulipwa kwa mujibu wa sheria za ununuzi wa umma.