Dondoo

Rudi kwenu utafute mahari tunayotaka, wazazi wa kidosho wafokea jombi

Na MWANDISHI WETU August 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KABATI, Murang’a:

KALAMENI aliyekutana na wazazi wa mpenzi wake katika eneo hili kupata baraka waoane, alijipata taabani walipomtaka kusitisha mipango ya harusi iwapo hana uwezo wa kutoa mahari iliyohitajika.

Kama ilivyo desturi kalameni pamoja na jamaa zake walikuwa wameenda kwa kina mrembo wake ili kujadili na wazazi wake kuhusu mahari.

“Sisi tumetoa matakwa yetu kwenu. Hatutaki mabishano. Iwapo hauna uwezo basi achana na harusi,” polo aliambiwa.

Duru zinasema polo na ujumbe wake walijaribu kuwashawishi wazazi wa mrembo wachukue kiwango cha mahari alichokuwa nacho lakini hawakutoboa.

“Hakuna mahali huyu msichana anaenda. Wewe rudi nyumbani na ukipata kiwango cha mahari tunachohitaji tuambie. Kwa sasa sahau harusi,” polo aliambiwa.