Mrengo mpya sasa waibuka Mlimani kumuunga mkono Ruto
HUKU vita vya kisiasa kudhibiti kura za eneo la Mlima Kenya vikizidi kushika kasi kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, mrengo wa tatu wa kisiasa unaohusishwa na Rais William Ruto umeibuka.
Mbunge wa Ndia George Kariuki, mshirika wa karibu wa Rais Ruto, ameanzisha kile anachokiita “vikao vya mashauriano” nyumbani kwake Gacharu.
Baada ya Rigathi Gachagua kung’olewa kutoka wadhifa wa Naibu Rais mnamo Oktoba 2024, alianza kampeni kali dhidi ya aliyekuwa bosi wake, akimlaumu kwa usaliti wa kisiasa.
Kupitia chama chake cha Democracy for Citizens Party (DCP), Bw Gachagua amekuwa akiendesha mikutano na kampeni katika kaunti mbalimbali za Mlima Kenya, hali ambayo karibu imefungia nje chama cha United Democratic Alliance (UDA).
Ushindi wa DCP katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol-Kalou, ambapo mgombea wake Kamau Ngotho alimshinda Muchina Nyaga wa UDA kwa zaidi ya kura 30,000, umempa nguvu zaidi Bw Gachagua, ambaye anadai ushindi huo ulikuwa kura ya kuamua kukataa Rais Ruto.
Mwezi Julai, Bw Gachagua alitangaza kujifungia kwa siku 45 katika makazi yake ya Wamunyoro, ambako amekuwa akipokea jumbe na viongozi kutoka maeneo mbalimbali ya Mlima Kenya, Nairobi na Bonde la Ufa. Hali hiyo imefanya Wamunyoro kuwa kitovu kikuu cha maamuzi ya kisiasa.
Kwa upande mwingine, Naibu Rais Kithure Kindiki pia amekuwa akitumia nyumbani kwake Irunduni kupokea viongozi kutoka eneo hilo kwa lengo la kupunguza ushawishi wa Bw Gachagua na kuimarisha uungwaji mkono wake.
Bw Kariuki amesema kwa siku 90 zijazo ataalika wakazi wa Mlima Kenya pamoja na maeneo mengine ya nchi kujadili mustakabali wa kisiasa wa eneo hilo kabla ya kutoa tamko ambalo ameliita “Azimio la Gacharu.”
Kauli zake alipokutana na viongozi wa wanawake kutoka eneo la Othaya Jumatatu zilitoa dalili za hatua zake za baadaye.
Wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa mbunge huyo anaandaliwa kuwa kiongozi wa kisiasa katika Mlima Kenya Magharibi na huenda akazingatiwa kama mgombea mwenza wa Rais Ruto mwaka wa 2027.
“Mwaka ujao nitakuwa nimetumikia wananchi wa Ndia kwa miaka kumi. Je, sifai kushikilia wadhifa mkubwa zaidi? Siwezi kushiriki siasa za kitaifa?” alihoji Bw Kariuki.
Aliwasihi wananchi kutochagua viongozi kwa misingi ya vyama vya kisiasa pekee bali kwa uwezo na kujitolea kwao kuhudumia wananchi.
Pia kuna madai kuwa anapigiwa upatu kuchukua nafasi ya mgombea mwenza wa Rais iwapo itaonekana ana uwezo mkubwa zaidi wa kuunganisha kura za Mlima Kenya kuliko Profesa Kindiki.
Alipoulizwa iwapo analenga wadhifa wa juu zaidi wa kisiasa, Bw Kariuki alikataa kuthibitisha azma yoyote ya kuwa Naibu Rais, akisema atatangaza msimamo wake baada ya kukamilisha mashauriano hayo.
Katika siku za hivi majuzi amekuwa akiongea kwa sauti kuhusu uongozi wa eneo hilo akisisitiza kuwa “Mlima Kenya unahitaji viongozi imara”, kauli ambayo wengi wametafsiri kuwa kukosoa Prof Kindiki ambaye bado hajafanikiwa kupunguza ushawishi wa Bw Gachagua.
Wakati huo huo, baadhi ya viongozi kutoka Mlima Kenya Mashariki, wakiongozwa na Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, wamekuwa wakishinikiza eneo hilo lichukue mkondo wake wa kisiasa tofauti na Mlima Kenya Magharibi.
Prof Kindiki amejipata katika hali ngumu kutokana na msimamo huo, huku akiendelea kutetea umoja wa eneo lote la Mlima Kenya.
Mlima Kenya Mashariki unajumuisha kaunti za Embu, Meru na Tharaka Nithi ambako Prof Kindiki anatoka, huku Kirinyaga, Nyeri, Murang’a, Nyandarua na sehemu za Laikipia zikihesabiwa kuwa Mlima Kenya Magharibi.
Bw Ruku anasema upinzani mkubwa dhidi ya Rais Ruto unatoka Mlima Kenya Magharibi na ameshutumu eneo hilo kwa kile anachokiita usaliti wa kisiasa.
Jumanne, Bw Ruku aliambia Taifa Leo kuwa yeye na Mbunge Kariuki wana mpango mkubwa wa kumsaidia Rais Ruto kupata takriban kura milioni tatu katika eneo la Mlima Kenya.