Habari za Kitaifa

Mama, mwanawe wadai kusingiziwa mauaji ya Dkt Mutiso ili mali yao ya Sh1.5bn itwaliwe

Na RICHARD MUNGUTI August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KULIKUWA na kizaazaa katika Mahakama ya Milimani baada ya Rose Mbithe Mulwa na mwanawe Chris Mulwa kudai wanasingiziwa kuhusika katika mauaji ya Dkt Victoria Mutiso ili mali ya familia ya thamani ya Sh1.5 bilioni itwaliwe.

Rose alidai hawezi kufikia akaunti zake za benki ili kupata pesa za matibabu na mahitaji ya kila siku.

Alitoa madai mazito dhidi ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP), akisema kesi dhidi yake imebuniwa.

Rose Mbithe Mulwa, anayeshukiwa kwa mauaji ya Dkt Victoria Mutiso. Picha|Richard Munguti

“Hawajawahi kuniona nikimuua Dkt Victoria Nthunya Mutiso,” Rose alidai.

Alisema alimsomesha aliyekuwa mumewe, Profesa David Ndetei, hadi kiwango cha uzamifu (PhD), na kwamba sasa ana matatizo makubwa ya kiafya.

Chris naye alidai maafisa wa DCI walimtisha ili aandike taarifa dhidi yake, la sivyo wangeomba mahakama iamuru azuiliwe kwa siku 60.

“Mimi ni wakili wa mahakama hii na nina haki ya kujieleza,” Chris alisema.