Habari za Kitaifa

Ruto azungumzia siku za mwisho na Raila akisema alimwambia alishatoka hospitali

Na JUSTUS WANGA August 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto ameeleza jinsi alivyopokea taarifa ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, mauti ambayo yalizua wingu la huzuni na kutumbukiza taifa kwenye wimbi la maombolezo.

Kwenye mahojiano na Taifa Leo, Rais Ruto alisema alikuwa akielekea afisini mwake mwendo wa saa 12:30 asubuhi Oktoba 15, 2025, simu yake ilipokereza. Simu hiyo ilipigwa na Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga, kakake mkubwa wa Bw Odinga.

“Kuna tatizo, ‘kiongozi wa vijana’ (Oburu) aliniambia. Nadhani nimempoteza kaka yangu,” Rais Ruto alikumbuka Dkt Oburu akisema.

Dkt Oburu hujiita “kiongozi wa vijana” licha ya umri wake pevu wa miaka 83.

Raila alikuwa amefariki India, ambako alikuwa ameenda kutibiwa akiwa na matumaini ya kupona na kurejea nchini.

Rais Ruto, alisema alikuwa amezungumza na Raila siku chache kabla ya kifo chake na akaambiwa alikuwa ametoka hospitalini na alikuwa akienda kupumzika.

Muda mfupi baadaye, dadake Raila, Ruth Odinga, pia alimpigia simu Rais Ruto simu. Familia ilimweleza kuwa Raila alikuwa ameamka asubuhi hiyo, akafanya mazoezi kabla hali yake kuzorota ghafla.

“Maisha yake hayakuweza kuokolewa,” Rais Ruto akasema akikumbuka kauli ya Ruth Odinga.

Rais Ruto na Raila walikuwa wamefahamiana kwa miongo kadhaa, wakati mmoja wakishirikiana kisiasa na mara nyingine wakitofautiana vikali na kila mmoja kuchukua mwelekeo wake.

“Tulianza tukiwa pande tofauti tulipokuwa Kanu, wao wakiwa Ford na wengine. Tulikutana ODM, tukaijenga pamoja. Nilijitahidi kumuunga mkono na alikuwa kiongozi mzuri wa kikosi chetu, kisha tukatengana tena,” akasema Rais Ruto.

Wawili hao walikabiliana katika uchaguzi wa urais wa 2022, ambapo Rais Ruto alishinda kwa kura 7,176,141 dhidi ya 6,942,930 za Raila.

Hata hivyo, maandamano ya 2024 yalibadilisha mazingira ya kisiasa na hatimaye makundi yao yakashirikiana katika Serikali Jumuishi, Raila akiwa sehemu ya serikali hiyo.

Rais Ruto alisema katika wiki za mwisho za maisha ya Raila, uhusiano wao ulikuwa umeimarika sana. Walipigiana simu, kukutana na hata kula chakula cha jioni nyumbani kwa Raila.

Aidha Rais Ruto alisema Raila alikuwa amepiga simu akisema hakuwa akijihisi vizuri na alitaka kumwona. Raila alimtembelea Rais katika Ikulu ya Nairobi na kujadili masuala mbalimbali kuhusu mustakabali wa nchi.

Baadaye, Rais Ruto alimtembelea Raila nyumbani kwake baada ya kuambiwa alikuwa amerejea Nairobi.

Walikula chakula cha jioni pamoja na Raila kumweleza kuwa alitaka kupata maoni ya pili ya madaktari kwa sababu afya yake haikuwa ikiimarika.

Raila baadaye alisafiri hadi India akiwa na binti yake, madaktari na wengine.

Wawili hao waliendelea kuwasiliana kwa simu.

Rais Ruto alisema Raila mwanzoni alikuwa na matumaini, akimweleza kuwa madaktari kadhaa walikuwa wamemchunguza na kuamini wamepata matibabu yaliyofaa.

Lakini siku chache baadaye, Rais alipokea habari kwamba Raila alikuwa ametoka hospitalini na alikuwa akipanga kupumzika.

Hiyo ndiyo ilikuwa taarifa ya mwisho aliyopokea Rais Ruto kabla ya simu ya Dkt Oburu kumjulisha kuhusu kifo cha Raila.

Baadaye Ruto alishiriki katika mipango ya kurejesha mwili wa Raila nchini, akiwemo kuwasiliana na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi, ambaye alisema alimfahamu Raila binafsi.

Kwa Rais Ruto, sehemu ngumu zaidi ilikuwa jinsi kifo hicho kilivyotokea ghafla, kwani siku chache tu kabla walikuwa wakijadili mustakabali wa Kenya.