Habari za Kitaifa

Shule za upili zalemaa mgao ukipungua nayo serikali ikionya walimu dhidi ya kuongeza karo

Na DAVID MUCHUNGUH, MERCY SIMIYU August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKUU wa shule za sekondari wameonya kuwa uhaba wa fedha unaathiri ubora wa elimu, huku wakitaka serikali iongeze kiwango cha fedha kinachotolewa kwa kila mwanafunzi.

Wakuu hao wamesema gharama ya kuendesha shule imeongezeka kwa kiasi kikubwa tangu kiwango cha ufadhili cha Sh22,244 kwa kila mwanafunzi kwa mwaka kilipowekwa mwaka 2014.

Onyo hilo linajiri shule zinapoanza muhula wa tatu, ambao ni muhimu kwa watahiniwa wa Kidato cha Nne wanaojiandaa kwa mitihani yao ya kitaifa (KCSE).

Kwa mujibu wa uchanganuzi wa Chama cha Wakuu wa Shule za Sekondari (KESSHA), shule zimepokea Sh16,056.29 kwa kila mwanafunzi mwaka huu, dhidi ya Sh22,244 zinazotarajiwa.

Hii inaacha pengo la Sh6,188 kwa kila mwanafunzi, sawa na asilimia 27.82 ya fedha zinazotarajiwa.

KESSHA ilisema shule zilipokea Sh7,952.04 kwa kila mwanafunzi katika muhula wa kwanza, Sh4,766.49 muhula wa pili na Sh3,337.76 mwanzoni mwa muhula wa tatu.

Mwenyekiti wa shule za kitaifa, Casper Maina, ambaye pia ni mkuu wa Nairobi School, alisema kiwango hicho hakikidhi mabadiliko ya gharama ya maisha.

“Mgao hautoshi. Kiwango hiki kiliwekwa mwaka 2014, miaka 12 iliyopita. Mambo mengi yamebadilika tangu wakati huo. Kwa nini hakiongezwi upya?” alisema.

KESSHA ilisema shule zilipokea Sh11,892.14 kwa kila mwanafunzi mwaka 2023, sawa na asilimia 53.46 ya kiwango kilichotarajiwa.

Mwaka 2024, kiasi hicho kiliongezeka hadi Sh16,205.96, sawa na asilimia 72.86, kabla ya kushuka hadi Sh15,385.12 mwaka 2025.

Mwaka huu, ingawa kiasi kilichotolewa kimeongezeka, bado shule hazijapokea fedha zote zinazotarajia.

Wakuu wa shule walisema wanakabiliwa na gharama kubwa za chakula, umeme, maji, usafiri na vifaa vya masomo na mishahara ya wafanyakazi wasio walimu.

“Tunatakiwa kutoa elimu bora kwa kutumia rasilimali ambazo hazijaongezeka kulingana na gharama. Mkuu wa shule analazimika kuamua ni jambo gani la kulipia sasa na lipi litasubiri,” alisema mkuu mmoja wa shule Nakuru.

Shule pia zinakabiliwa na gharama ya maandalizi ya mtihani wa KCSE, ikiwemo ununuzi wa kemikali, vifaa vya maabara na uchapishaji wa mitihani ya marudio.

Mkuu mwingine wa shule Nairobi alisema baadhi ya shule zimeanza kutegemea kukopa toka kwa wasambazaji.

“Tunakopa na kuwaomba wasambazaji watupatie muda zaidi. Lakini huwezi kuendelea kukopa milele,” alisema.

Wakati huo huo, Waziri wa Elimu, Bw Julius Ogamba amewataka wakuu wa shule kutumia fedha za umma kwa uangalifu na kuacha kuwatoza wazazi ada zisizoidhinishwa.

“Serikali imejitolea kutekeleza wajibu wake kwa wanafunzi na taasisi za elimu,” alisema.