Habari za Kitaifa

Rais kukita kambi Kajiado siku 3 kukagua miradi na kupigia debe ‘rekodi yake ya maendeleo’

Na JUSTUS OCHIENG September 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto ameanza ziara ya siku tatu katika Kaunti ya Kajiado, hatua inayotafsiriwa na wachambuzi kama juhudi za kuimarisha maendeleo na wakati huo huo kujiweka katika nafasi nzuri kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Rais anatarajiwa kuzuru maeneo mbalimbali ya Kajiado kati ya jana Septemba 3 na Septemba 7 kukagua na kuzindua miradi ya umeme, barabara, unyunyuzaji, masoko ya kisasa, nyumba za gharama nafuu na mabweni ya wanafunzi.

Ingawa ziara hiyo imewasilishwa kama ya maendeleo, wengi wanasema ina uzito wa kisiasa kutokana na umuhimu wa kura za jamii ya Maa inayopatikana hasa katika kaunti za Kajiado, Narok na Samburu.

Kaunti hizo tatu zina zaidi ya wapigakura milioni 1.09 waliosajiliwa.

Ziara hiyo imejiri wiki chache baada ya Rais Ruto kufanya ziara ya siku mbili Narok, ambapo alizindua miradi kadhaa ya maendeleo na kusisitiza ushirikiano kati ya UDA na ODM.

Akiwa Narok, Rais alisema kuwa hapo awali kura za eneo hilo zilikuwa zikigawanywa kati yake na aliyekuwa kiongozi wa ODM, Raila Odinga, lakini sasa ana matumaini ya kupata uungwaji mkono mkubwa kutokana na ushirikiano wa vyama hivyo viwili.

Akiwa Kajiado, Rais atakagua miradi mbalimbali ikiwemo soko la kisasa la Kimana, mpango wa nyumba za bei nafuu Oloitoktok, mradi wa umeme wa Sultan Hamud-Loitoktok, masoko Namanga na Kajiado Town pamoja na miradi ya maji na barabara.

Hata hivyo, Rais anakabiliwa na ushindani kutoka kwa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) kinachoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Bw Gachagua amekuwa akifanya ziara za mara kwa mara katika maeneo ya Maa akijaribu kuvutia viongozi na wapigakura wa eneo hilo.

Kwa zaidi ya wapigakura nusu milioni Kajiado pekee, eneo hilo linaonekana kuwa uwanja muhimu wa mapambano ya kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027.

Wachambuzi wanasema ziara ya Rais ni uwekezaji wa mapema wa kisiasa pamoja na juhudi za kuonyesha rekodi ya maendeleo ya serikali yake.