Hospitali zakwama Serikali ikilaumiwa kupuuza matatizo yanayolemaza idara ya Afya
SERIKALI imelaumiwa kwa kupuuza sekta ya afya ya umma iliyoathiriwa na mgomo wa wauguzi huku ikishughulikia sekta nyingine na kuacha wagonjwa kuteseka.
Wakati wafanyakazi wa sekta ya usafiri wa anga walipogoma Agosti 30 na kutatiza shughuli katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) pamoja na viwanja vya ndege vya Moi, Eldoret na Kisumu, serikali ilichukua siku mbili pekee kufanya mazungumzo na kutia saini makubaliano ya kurejea kazini.
Kufikia Septemba 1, mgomo ulikuwa umemalizika na safari za ndege kurejea kawaida.
Lakini kwa upande mwingine, wauguzi wamekuwa mgomoni kwa siku 39 huku maafisa wa maabara, afya ya umma, lishe, wafamasia, maafisa wa utabibu na wahudumu wa Mpango wa Afya kwa Wote (UHC) wakiendelea kugoma kwa karibu siku 50.
Katika kipindi hicho, akina mama wamekuwa wakifariki wakiwa wodini wakijifungua, watoto wachanga wakipoteza maisha kabla hata ya kupumua kwa mara ya kwanza, huku serikali ikikosa kufikia makubaliano yoyote na wahudumu wa afya.
Rais wa Chama cha Kitaifa cha Wauguzi nchini (NNAK), Collins Ajwang alisema, hatua ya haraka iliyochukuliwa na serikali kumaliza mgomo wa wafanyakazi wa anga inaonyesha tofauti ya namna sekta ya afya inavyoshughulikiwa.
“Tulianza kushinikiza utekelezaji wa Mkataba wa Pamoja wa Mishahara (CBA) pamoja na madaktari na maafisa wa utabibu. Wao walipata mikataba yao na hata wakalipwa. Serikali inasema wauguzi ni wengi hivyo haina bajeti ya kutulipa. Hiyo haina mantiki kwa sababu idadi yetu kubwa ndiyo imewezesha hospitali kufanya kazi ipasavyo,” alisema Ajwang.
Katibu Mkuu wa Muungano wa Wauguzi Kenya (KNUN), Seth Panyako, alisema suala hilo linahusu maslahi na vipaumbele vya serikali.
“Walio madarakani wanaweza kwenda hospitali za kibinafsi. Lakini mwananchi wa kawaida hutegemea hospitali za umma. Hali hii inaonyesha wazi kuwa hawajali afya ya wananchi wa kawaida,” alisema.
Takwimu kutoka mfumo wa Every Woman, Every Newborn, Everywhere (EWENE) zinaonyesha hali ya janga hilo.
Kati ya Jumatatu na Alhamisi wiki hii pekee, wanawake wanane walifariki kutokana na matatizo ya uzazi, watoto wachanga 16 walio na chini ya mwezi mmoja walikufa na vifo 55 vya watoto wa kipindi cha kujifungua vilirekodiwa.
Mwezi uliopita pekee, wanawake 75 walifariki kutokana na matatizo ya uzazi huku watoto 458 wakifariki kabla au mara tu baada ya kuzaliwa.
Ajwang alisema kaunti za Kisumu, Nakuru, Kakamega na Kajiado zimeathirika zaidi.
“Hakuna dalili kuwa hali inaimarika. Wanawake wengi sasa hawafiki hospitalini. Wanaojifungulia nyumbani au maeneo yasiyo rasmi hawahesabiwi katika takwimu hizi,” aliongeza.
Kwa mujibu wa vyama vya wahudumu wa afya, mgomo huo umeathiri pia mafunzo ya wanafunzi wa uuguzi, udaktari na maafisa wa utabibu ambao hutegemea hospitali za umma kupata ujuzi.
“Wauguzi ni karibu asilimia 70 ya wafanyakazi wote wa afya nchini. Kutokuwepo kwao hospitalini si suala la mzozo wa wafanyakazi pekee tena. Sasa ni suala la usalama wa wagonjwa na afya ya umma,” alisema Ajwang.
Chanzo kikuu cha mgogoro huo ni utekelezaji wa CBA ambayo wauguzi wamekuwa wakidai tangu 2017.
Ingawa mgomo wa miezi sita mwaka huo ulisitishwa baada ya makubaliano ya kurejea kazini, viongozi wa vyama vya wafanyakazi wanasema hadi leo CBA hiyo haijatekelezwa kikamilifu.
Wauguzi wanashutumu Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC), Wizara ya Afya na Baraza la Magavana kwa kuchelewesha hatua zinazohitajika ili mkataba huo usajiliwe na kutekelezwa.
Akizungumza wakati wa maandamano katika ofisi za SRC, Panyako alisema maafisa wa tume hiyo walifunga ofisi zao na kuondoka kabla ya kukutana na wauguzi.
“Tumekuwa wavumilivu kwa zaidi ya miaka tisa. Serikali haiwezi kuendelea kutupa ahadi halafu ishindwe kuzitimiza ilhali wauguzi ndio wanaobeba mzigo mkubwa katika hospitali nyingi za umma,” alisema.
Hata hivyo, alisema kuna maendeleo katika mazungumzo kuhusu mwongozo wa maendeleo ya taaluma na ajira za kudumu kwa wafanyakazi wa UHC.
Kwa sasa, suala kubwa lililosalia ni kutiwa saini kwa CBA.
Panyako pia alitaka mfumo wa usimamizi wa wafanyakazi wa afya uwe wa kitaifa badala ya kuachwa mikononi mwa kaunti pekee.
“Hauwezi kufanikisha Afya kwa Wote bila kuwa na mfumo wa pamoja wa kusimamia wahudumu katika sekta ya afya,” alisema.
Ajwang alitoa wito kwa serikali ya kitaifa, serikali za kaunti, vyama vya wafanyakazi na wadau wengine kuketi pamoja na kutatua mgogoro huo haraka.
“Kila siku ya kuchelewa inamaanisha maisha zaidi yanapotea. Wauguzi wanataka kurejea hospitalini ili Wakenya wapate huduma wanazohitaji,” alisema.